Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imeliomba Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuidhinisha kiasi cha Sh.4.2 trilioni, huku kiasi cha sh 1.5 trilioni zikilenga kujenga reli ya kisasa (SGR).

Maombi hayo ya wizara kupitia bajeti ya Mwaka wa Fedha 2018/19, yaliwasilishwa bungeni hapo na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Profesa Makame Mbarawa, wakati wa kuwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo.

“Serikali imetenga sh 1.5 trilioni ambazo ni fedha za ndani kuendelea na ujenzi wa reli ya kati ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro, yenye urefu wa kilomita 300, na Morogoro hadi Makutupora, yenye urefu wa kilomita 422), na sh1.4 trilioni zitatumika,” alisema Profesa Mbarawa.

Aidha, alisema kuwa Serikali imetenga sh495 bilioni kwa ajili ya kununua ndege mbili, moja aina ya Bombardier Q400  na nyingine aina ya Boeing 787-8 (Dream liner) yenye uwezo wa kubeba abiria 262. Hiyo ni sehemu ya jitihada za kuiwezesha zaidi Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL).

Katka maelezo yake, alisema kuna fedha zilizotengwa kwa ajili ya upanuzi wa barabara ya Mwenge-Morocco, ukarabati wa barabara kuu na barabara za mikoani pamoja na upanuzi wa viwanja vya ndege.

Ujenzi wa reli ya Mtwara-Mbambabay na matawi ya Mchuchuma na Liganga pia yametengewa kiasi cha sh1.5 bilioni.

Wananchi Njombe waiomba Serikali kukamilisha ujenzi ghala la matunda
Fatuma alia na uhaba wa mawakili, wakili mmoja wateja 25,000