Mshambuliaji wa klabu inayoshikilia usukani wa msimamo wa ligi ya nchini England, Leicester City, Riyad Mahrez usiku wa kuamkia leo ameshinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Mwaka wa Chama cha Wachezaji wa Kulipwa (PFA) katika Ligi Kuu ya soka nchini humo.

Mahrez amekuwa na msimu mzuri kwa vinara hao wa Ligi Kuu ya England- hadi sasa akiwa amefunga mabao 17 na kuseti 11.

Mwanasoka huyo wa kimataifa wa Algeria, ambaye amekuwa chachu ya mafanikio kwa mabingwa hao watarajiwa England, alikabidhiwa tuzo yake katika ukumbi wa hoteli ya Grosvenor Hotel mjini London na kuwashukuru wachezaji wenzake.

“Sifa zote zinakwenda kwao, kabisa, na kwa kocha na benchi la ufundi. Bila wao nisingepokea tuzo hii na nisingefunga. Ni hamasa ya timu, na ninataka kuilekeza kwao,” amesema Mahrez akiwashukuru wachezaji wenzake wa Leicester kwa mafanikio yake.

Mahrez amekuwa na mchango mkubwa kwa timu yake na sasa anaungana na washindi wa awali wa tuzo hiyo wakiwemo Kenny Dalglish, Dennis Bergkamp, Thierry Henry, Cristiano Ronaldo na Gareth Bale.

Kikosi cha Claudio Ranieri kinahitaji angalau pointi tano katika mechi zake tatu zilizobaki ili kutawazwa kuwa mabingwa wapya wa England kwa mara ya kwanza katika historia yao.

Mahrez pia alifunga katika mchezo wa Ligi Kuu usikubwa jana Uwanja wa King Power, Leicester wakiitandika Swansea 4-0 kabla ya kukumbizwa kwenye sherehe za tuzo kwa helikopta baada ya mechi.

Mshambuliaji huyo amewapiku wachezaji mwenzake wa Leicester, Jamie Vardy na N’Golo Kante katika kinyang’anyiro cha tuzo hiyo sambamba na mshambuliaji wa Tottenham, Harry Kane, kiungo wa Arsenal, Mesut Ozil na wa West Ham, Dimitri Payet.

Vardy ameshika nafasi ya pili katika kura, wakati Kane amekuwa wa tatu. Mshambuliaji huyo wa Leicester pia alipewa tuzo maalum kwa kuvunja rekodi ya kufunga mabao katika mechi 11 mfululizo.

Donald Trump: Nikishindwa Hamtaniona Tena
Kangi Lugola amtega Rais Magufuli