Rapa 50 Cent amechoma moto nguo zake za kifahari za kampuni ya Gucci kama ishara ya kupinga kitendo cha ubaguzi wa rangi kilichofanywa na kampuni hiyo kupitia picha/sanamu yake ya hivi karibuni.

Gucci walitoa picha inayomuonesha mtu mwenye sura ya ‘kizungu’ lakini amevalia sweta linalomzidi pamoja na mdomo wenye rangi nyekundu uliopambwa kihorera, picha iliyokosolewa vikali kuwa inawashambulia watu weusi.

Akichoma fulana yake ya Gucci aliyoinunua $480, rapa huyo mtata amesema kuwa ameachana kabisa na nguo za kampuni hiyo alizonazo.

“Nimeachana rasmi na nguo za Gucci nilizonazo nyumbani. Siungi tena mkono biashara yao,” aliandika kwenye video hiyo.

Kiongozi huyo wa G-Unit alieleza kuwa ana mpango wa kugawa nguo hizo kwa watu wanaoishi kwenye mazingira magumu na wasio na makazi.

Mbali na 50 Cent, rapa Soulja Boy ambaye ni mpenzi mkubwa wa Gucci pia ametangaza kuachana na mavazi ya kampuni hiyo akidai kuwa ameyasimamisha hadi atakapotoa  taarifa. T.I na mkewe Tiny pia ni kati ya watu maarufu waliopinga vikali kitendo hicho cha Gucci.

Hata hivyo, Bondia Floyd Mayweather yeye ametofautiana na wasanii hao, akifanya manunuzi kwenye duka la Gucci na kueleza kuwa hajali kinachoendelea.

Kampuni hiyo maarufu ya nguo za kifahari imeomba radhi na kueleza kuwa picha/sanamu hiyo imeondolewa rasmi kwenye maduka yao ya mtandaoni pamoja na maduka ya kawaida.

Serikali kujenga mazingira wezeshi katika sekta ya kilimo
Wanafunzi walioongoza mtihani kidato cha nne watoa neno