Beki kutoka nchini Qatar Abdelkarim Hassan ametajwa kuwa mchezaji bora wa mwaka wa bara la Asia, katika hafla maalum zilizofanywa na shirikisho la soka barani humo (Asian Football Confederation) ASF, mjini Muscat nchini Oman usiku wa kuamkia leo.

Abdelkarim ametajwa kuwa mshindi wa tuzo hiyo, na kuwapiku waliokua wapinzani wake kutoka nchini Japan Yuma Suzuki na Kenta Misao.

Beki huyo wa upande wa kushoto anaitumikia klabu ya Al Sadd SC ya nchini kwao Qatar, ambayo aliisaidia kufika hatua ya nusu fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Asia msimu huu.

Baada ya kutangazwa na kupokea tuzo ya mchezaji bora wa mwaka barani Asia Abdelkarim mwenye umri wa miaka 25 alisema: “Ninafuraha ya kufikia mafanikio haya, sina budi kuwashukuru wachezaji wenzangu na viongozi wa Al Sadd SC, kwa ushirikiano walionipa hadi leo nimetangazwa kuwa mchezaji bora,”

“Kila mchezaji barani Asia ana ndoto ya kutwaa tuzo hii, lakini mwaka huu imekua bahati yangu, hatua ambayo ninaamini ni heshima kwa nchi yangu ya Qatar na watu wangu wote wa karibu.” Aliongeza Abdelkarim ambaye anakuwa mchezaji wa pili kutoka Qatar kutwaa tuzo ya mchezaji bora, baada ya Khalfan Ibrahim aliyefanya hivyo mwaka 2006.

Kiungo Wang Shuang naye alitangwazwa kuwa mshindi wa tuzo ya mchezaji bora wa mwaka upande wa wanawake, na kuwa mchezaji watatu kutoka China kufikia mafanikio hayo, akitanguliwa na Ma Xiaoxu na Bai Jie.

Makoto Hasebe, ambaye aliiongoza Japan kwenye hekaheka za kombe la dunia na kuishia hatua ya 16 bora, ametajwa kuwa mchezaji bora wa mwaka wa kimataifa, huku kocha wa timu ya taifa ya nchi hiyo Go Oiwa akishinda tuzo ya kocha bora wa mwaka kwa wanaume.

Kocha wa timu ya taifa ya wanawake ya Japan Asako Takakura, naye ametajwa kuwa kocha bora wa mwaka kwa wanawake, na kufikisha idadi ya kuchukua tuzo hiyo mara sita.

Ukraine yaiomba Nato kuingilia kati mgogoro wake na Urusi
Kilo moja ya Korosho yasababisha mwanafunzi kubakwa