Jeshi la polisi nchini limetofautiana katika taarifa zake kuhusu kupatikana kwa Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo ambapo RPC wa Iringa alisema kijana huyo alifika mwenyewe kituo cha polisi huku Mambosasa akipinga hilo.

Katika taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Juma Bwire Machi 8, 2018 imeonyesha kutofautiana na kauli iliyotolewa jana Machi 13, 2018 na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa,

“Jana tarehe 7 mwezi wa tatu majira ya saa moja Abdul Nondo alifika katika kituo cha polisi Mafinga wilaya ya Mufindi na kuelezea kuwa ametekwa na watu wasiofahamika, jeshi la polisi mkoa wa Iringa limefungua jalada la uchunguzi ili kubaini ukweli kama alikuwa ametekwa na kama kweli alikuwa ametekwa tunaahidi kwamba sisi jeshi la polisi tukiwapata watuhumiwa sheria itachukua mkondo wake,”amesema Kamanda Bwire

Hata hivyo, katika taarifa iliyotolewa Kamanda wa polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, Lazaro Mambosasa imesema kuwa kijana huyo alikamatwa na polisi akiendelea na shughuli zake na wala hakuripoti sehemu yeyote.

 “Kijana huyo alikamatwa na jeshi la polisi na wala hakuripoti mahali popote si kwa Mwenyekiti wa Mtaa, si kwa Afisa Mtendaji wa Kata, wala kituo chochote cha polisi mkoani Iringa bali alikamatwa akiwa Mafinga akiendelea na shughuli zake,”amesema Kamanda Mambosasa

 

Magufuli awasha moto TRA, awapa onyo kali
Mradi bomba la mafuta Hoima kugawa ajira 10,000 kwa watanzania