Wekundu Wa Msimbazi Simba wanatarajiwa kuondoka nchini Jumatano ili kuifuata Al Masry nchini kwao, huku wakihitaji ushindi wa aina yoyote katika mechi yao ya marudiano ya Kombe la Shirikisho Afrika na habari njema ni kwamba, aliyekuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage ameamua kujitosa kuanika siri kubwa ya kuweza kupata ushindi ugenini.

Rage enzi akiwa kiongozi mkubwa Msimbazi waliwahi kuing’oa Es Setif ya Algeria, amewaambia Simba wasikubali kuandaliwa kitu chochote na wenyeji wao bali waombe msaada kutoka Ubalozi wa Tanzania uliopo Misri vinginevyo watachemka vibaya.

Simba ililazimishwa sare ya mabao 2-2 na Al Masry kwenye mchezo wa awali jijini Dar es Salaa na hivyo, wanahitaji ushindi wa aina yoyote ili kusonga mbele.

Rage alisema ana mpango wa kuzungumza na viongozi wa Simba ili kuwapa mbinu za ushindi. Pia alisema endapo kutakuwa na umbali wa Km200 kutoka Cairo hadi Port Said utakapochezwa mchezo huo, Simba wana haki ya kugoma kupanda basi na badala yake kupanda ndege kwa mujibu wa kanuni za mashindano hayo.

“Naipenda sana Simba na kama nitakuwepo Dar es Salaam nitakwenda Misri kuwasapoti wachezaji na viongozi kwenye mchezo huo muhimu. Ila kikubwa Simba wasikubali kufanyiwa maandalizi na wenyeji wao. Hapo watafanikiwa kuepuka figisufigisu.

“Nitazungumza na viongozi ili wafanye mawasiliano na Ubalozi wa Tanzania nchini Misri, wawasaidie kufanya maandalizi yote muhimu ikiwemo mapokezi kutoka uwanja wa ndege kwenda hotelini na baadaye kwenda kwenye mchezo huo bila wenyeji kuhusika.

“Pia wasikubali kupanda gari sehemu ambayo ina umbali wa Km200, zikiwa chini ya hapo wanapaswa kupewa usafiri wa basi ambalo halitawachosha hiyo ni sheria kabisa na ipo wazi,” alisema Rage ambaye amewahi kuwa Mbunge wa Tabora Mjini.

UN yawapa tano Uhuru Kenyatta na Raila Odinga
Trump amfukuza kazi Waziri wa Mambo ya Nje