Agizo la Rais wa Uganda, Yoweri Museveni kwa timu ya taifa ya nchi hiyo, Uganda Cranes kuhakikisha inaifunga Taifa Stars licha ya kujihakikishia kufuzu kushiriki Fainali za Kombe la Mataifa Huru Barani Afrika (Afcon), limeibua gumzo la utani wa aina yake.

“Hata kama Uganda Cranes tayari wameshafuzu [Afcon], najua kuwa wana mechi dhidi ya Tanzania. Tafadhali hakikisheni hampotezi mchezo huo. Hongereni tena.

Kupitia mitandao ya kijamii, Watanzania wamejitokeza kumjibu Rais Museveni, akiwemo mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe ambaye ametumia utani kumkumbusha kuwa bomba la mafuta na gesi kutoka nchini kwao limepitia Tanzania.

“Mzee acha roho mbaya. Mmeshasahau mafuta yenu yanapita Tanzania? Shauri yako,” aliandika Zitto.

Majibu hayo ya Zitto yaliwaibua wengine ambao walikuja na utani wao kivingine.

“Mh. kumbuka tulikuhifadhi kijijini kwa Mzee wangu Rugambwa pale Muhutwe – Bukoba. Huu ndio wakati wako wa kulipa fadhila cause hatukukudai hata thumni,” aliandika Liliaruga, na kuongeza “Webalinyo! Kalessebo! Banangeee! Kura za Watanzania tutakupa uwe President wa EA.”

Mwingine aliandika, “Hahaha Mzee kamaanisha vice versa ili Fifa wasielewe… Mambo ya Fair play.”

Taifa Stars wanategemea zaidi ushindi wa mechi dhidi ya Uganda Cranes kupata matumaini ya kufuzu kushiriki Afcon nchini Cameroon, baada ya kupoteza 1-0 dhidi ya Lesotho.

Uganda wanaongoza kundi wakiwa na alama 13 huku Tanzania ikiwa na alama 5. Kwa hali ilivyo, wakati Tanzania wakitakiwa kushinda mechi dhidi ya Uganda, wanaendelea kuziombea njaa zaidi Lesotho na Cape Verde.

Arsenal kusaka mshambuliaji Januari 2019
Neymar, Mbappe waiweka njia panda PSG