Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amezindua soko kuu la dhahabu mkoa wa Geita ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alilotoa Januari 22, jijini Dar es Salaam mwaka huu kupitia mkutano wake na wafanyabiashara wa madini.

Waziri Majaliwa amezindua soko hilo leo Machi 17, 2019 ambapo katika hafla hiyo ameambatana na Waziri wa Madini, Dotto Biteko pamoja na watendaji mbalimbali wa taasisi mbalimbali za serikali.

Kabla ya uzinduzi Waziri Mkuu ametembelea na kuhoji masuala mbalimbali katika banda la Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), litakalotoa huduma mbalimbali ikiwamo uthibitishaji wa thamani halisi ya mapato yatokanayo na madini kwa wauzaji wa madini.

Pia ametembelea banda la kamati ya ulinzi na usalama kwa ajili ya kuimarisha usalama kwa wafanyabiashara na wadau wa soko hilo, na katika mabanda ya benki za NMB na CRDB zilizojipambanua namna zitakavyohusika katika ufanikishaji wa huduma za kifedha ndani ya soko hilo.

Soko hilo limetajwa kuwa litafungua fursa za kiuchumi kwa mkoa huo, ambapo litahusisha wadau wote walio kwenye biashara ya madini wakiwemo wanunuzi, wauzaji, TRA, Tume ya Madini, benki na mamlaka ya serikali za mitaa.

Awali, mkuu wa mkoa wa Geita, Robert Gabriel alisema mkoa huo unaongoza kwa uzalishaji wa dhahabu kwa zaidi ya asilimia 40 ya dhahabu yote inayozalishwa nchini.

Ombi la Mbunge Msukuma kwa Waziri Mkuu, 'Yasijengwe masoko mengine mikoani'
Majaliwa awatahadharisha wadau wa madini, 'Hatua kali za kisheria zitachukuliwa'