Mtu mmoja aliyetambulika kwa jina la Maricha Mniko(30) Mkurya dereva na mkazi wa Tandala Wilayani Makete anashikiliwa na jeshi la polisi Mkoani Njombe kwa tuhuma za kujifanya ni Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, IGP Simon Sirro ili kumsaidia ndugu yake kupata kazi katika kampuni ya magari ya Japanisee.
Hayo yamesemwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Renata Mziga ambapo amesema kuwa tukio hilo limetokea Mei 18 mwaka huu ambapo mtuhumiwa anadaiwa kumpigia simu Daniel Junishi mmiliki wa kampuni ya magari ya Japanisee.
Kamanda Mziga amesema kuwa baada ya kumpigia mtuhumiwa huyo inadaiwa alijitambulisha kuwa ni mkuu wa jeshi la polisi nchini hivyo anatakiwa amwajili mdogo wake aliyeko mkoa wa Mara.
“Baada ya kumwambia huyu mmiliki wa magari ya Japanisee alimuuliza kuwa namba yangu umeipata wapi akajibu nimepewa na Kamanda wa Polisi Mkoa Njombe na akasema yupo Dodoma,”amesema Kamanda Mziga.
Aidha, Kamanda Mziga ametoa rai kwa wananchi Mkoani humo kuwafichua watu wanaopiga simu kwa kutumia majina ya viongozi kwa maslahi yao binafsi.
Hata hivyo,katika hatua nyingine Kamanda Mziga amethibitisha kuokotwa kwa mwili wa mtu mmoja aliyetambulika kwa jina la Isack Mwambipile(27) amekutwa amekufa na kutupwa pembeni ya barabara baada ya kudaiwa kuvunja banda la kuku na kuiba.

Video: Majaliwa atoa maagizo mazito kwa Wakurugenzi
Nyota wa Chelsea watemwa kikosi cha taifa Spain