Aliyekua beki kutoka nchini Ufaransa Jean Alain Boumsong amejiunga na benchi la ufundi la timu ya taifa ya Cameroon (Indomitable Lions), kwa ajili ya kuongeza chachu kwa taifa hilo ambalo litakua mwenyeji fainali za Afrika za 2019.

Boumsong ambaye ni mzaliwa na Cameroon atafanya kazi na kocha mkuu Clarence Seedorf pamoja na msaidizi mwenzake Patrick Kluivert.

Mbali na wawili hao kutoka Uholanzi, pia Boumsong atafanya kazi na mshambuliaji wa zamani wa kikosi cha Cameroon Joel Epalle pamoja na Bill Tchato ambao wanaunda benchi la ufundi la kikosi Cameroon.

Epalle mwenye umri wa miaka 40, alishinda medali ya dhahabu akiwa na kikosi cha Cameroon kwenye michuano ya Olimpiki iliyofanyika mjini Sydney-Australia mwaka 2000, na miaka miwili baadae alikuwa miongoni mwa wachezaji waliotwaa ubingwa wa Afrika.

Kwa sasa Epalle  ni kocha msaidizi wa kikosi cha Cameroon sambamba na Patrick Kluivert wakimsaidiana Clarence Seedorf.

Kwa upande wa Bill Tchato ametajwa kama meneja wa timu ya taifa ya Cameroon.

Hata hivyo hii si mara ya kwanza kwa Boumsong mwenye umri wa miaka 38 kufanya kazi chini ya shirikisho la soka nchini Cameroon (Fecafoot), kwani amekua sambamba na uongozi wa shirikisho hilo tangu mwezi Juni  mwaka huu.

Alikua miongoni mwa wajumbe wa kamati iliyopewa kazi ya kujenga misingi na mikakati ya kuiwezesha timu ya taifa ya nchi hiyo kufanya vizuri, sambamba na kuweka mfumo wa benchi la ufundi litakavyokua, kabla ya kuajiriwa kwa Clarence Seedorf.

Boumsong alizaliwa mjini Douala na aliondoka nchini Cameroon akiwa na umri wa miaka 27 na kutimkia Ufaransa.

Kikosi cha Cameroon kwa sasa kinajiandaa na mchezo ya kimataifa wa kirafiki dhidi ya timu ya taifa ya Visiwa vya Comoros utakaochezwa mjini Mitsamiouli Septemba 08.

LIVE: Rais Magufuli akihutubia wananchi wa Butiama
Trump aagiza kukamatwa kwa Mwandishi anayekosoa Serikali yake