Hatimaye kitandawili kuhusu taarifa ya King Kiba kufunga ndoa na mrembo wa Mombasa Kenya kimeteguliwa baada ya mama mzaa chema kuzungumza akiwa harusini.

Sauti ya mama wa mrembo Aminah ambaye ndiye mke rasmi wa Ali Kiba imesikika jana kupitia redio maarufu zaidi jijini Mombasa ijulikanayo kama Pilipili FM.

Mama Aminah aliyeweka wazi kuwa yuko kwenye harusi ya mwanaye anayefunga ndoa na Ali Kiba ilitoa picha ya shangwe ya moyoni aliyokuwa nayo kuhusu tukio hilo.

“Tunasherehekea harusi ya mtoto wangu anaolewa na Ali Kiba. Namshukuru Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu atupe furaha, analopanga ni Mwenyezi Mungu,” alisikika mama akiongea moja kwa moja na mtangazaji wa Pilipili FM, Mgenge.

“Hata kama Ali Kiba anatoka TZ, lakini Mungu ndiye ameshapanga na tunampokea kwa mikono miwili. Mwanangu anaitwa Aminah,” aliongeza.

Hata hivyo, ndoa hiyo bado inaonekana kugubikwa na hali ya usiri kwa upande wa Ali Kiba ambaye hajaweka wazi kama tayari ameshafunga ndoa au bado yuko kwenye maandalizi, kupitia kurasa zake za mitandao ya kijamii.

Jana, mkali huyo wa ‘Seduce Me’ aliweka wazi kuwa alimtembelea rais mstaafu, Jakaya Kikwete ambapo pamoja na mambo mengine alimueleza kuwa anafunga ndoa hivi karibuni.

Kikwete pia aliweka picha ya Ali Kiba kwenye akaunti yake ya Twitter na kueleza kuwa amempa nasaha zake mwimbaji huyo kuhusu ndoa anayotarajia kufunga hivi karibuni.

Huenda kilichofanyika Mombasa ni ‘Send Off’, na kinachosubiriwa Tanzania ni ‘Harusi Kamili’ ya kumpokea mwali, kama ilivyokuwa kwa AY alipoanzia Rwanda na kukamilisha shamrashamra za ndoa nchini.

 

Magazeti ya ndani na nje ya Tanzania leo Aprili 15, 2018
Kikwete ampa neno Alikiba kuhusu ndoa yake