Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Ojo jijini Lagos nchini Nigeria, imemuachia huru Joseph Adetunji aliyekiri kummwagia tindikali usoni mtoto wake wa kiume wa kumzaa, baada ya kuridhishwa na utetezi wake.

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na mwendesha mashtaka, Uche Simeon, mshtakiwa alitenda kosa hilo Agosti 2015 katika mji mdogo wa Festac jijini Lagos, kutokana na ugomvi wa kifamilia.

Hata hivyo, Mahakama hiyo wiki hii iliridhishwa na sababu alizozitoa mshtakiwa kuwa alimmwagia tindikali kijana wake kwa lengo la kujilinda au kujihami.

“Mwanangu Adesoji ni mpumbavu katika familia yetu, na mara kadhaa amefanya jaribio la kutaka kuniua ili aweze kuridhi mali zangu,” Adetunji aliieleza mahakama katika utetezi wake.

Mshitakiwa huyo aliionesha mahakama makovu kadhaa mkononi ambayo alidai yalitokana na kushambuliwa na kijana wake huyo.

Alieleza kuwa alifanya kazi kubwa kuwasomesha watoto wake wa kiume kwenye shule nzuri na vyuo vizuri lakini huyo alishindikana na kugeuka kuwa mlevi na mkorofi, tofauti na kaka yake ambaye ni mwanasheria.

Alisema kuwa siku ya tukio, kijana wake huyo alimkuta akiwa anamsaidia mwanae wa kike kutengeza gari upande wa injini nyumbani kwake. Alisema alipofika alimtaka ampe fedha na akatishia kumdhuru.

“Alinifuata akiwa na chupa iliyopasuka akitishia kunichoma huku akitaka nimpe fedha, kwa kujihami nikamwagia maji ya betri (tindikali),” aliieleza Mahakama.

Aidha, hakimu A. Adesanya aliyesikiliza shauri hilo alieleza kuwa ugomvi huo wa kifamilia ulikuwa umefika mbali na kwamba mshitakiwa alipaswa kuwa ametoa taarifa polisi mapema kuhusu mashambulizi ya awali ya mwanaye dhidi yake.

Apigwa risasi kichwani wakijaribu kushuti video waweke Facebook
Rick Ross awatuliza mashabiki wa Diamond