Bingwa wa masumbwi wa dunia wa uzito wa juu, Anthony Joshua aliendeleza rekodi ya kutopigwa katika mapambano yake 22, lakini alitolewa kijasho kizito na mbabe kutoka Urusi, Alexander Povetkin.

Akipambana mbele ya mashabiki 80,000 katika uwanja wa wa mpira wa Wembley nchin Uingereza, Joshua alionekana kuwa katika wakati mgumu kwa alama dhidi ya Povetkin katika raundi za awali.

Uwezo wa Povetkin (39) na nguvu aliyoionesha ilimfanya kutawala sehemu ya mchezo katika raundi kadhaa, akitumia uzoefu wake akimchana Joshua puani na sehemu ya jicho kwa makonde mazito.

 

Hata hivyo, upepo ulionekana kumuishia Povetkin, na Joshua aliitumia nafasi hiyo kumzimisha kwa masumbwi mfululizo katika raundi ya 7.

Povetkin alipokea kipigo cha kwanza mwanzoni mwa raundi hiyo na kujikuta akiweka kichwa chake katikati ya kamba huku akihangaika kuamka, lakini alifanikiwa. Baada ya kipigo hicho, Joshua alifanikiwa kummalizia kwa masumbwi mengine mfululizo.

Hali hiyo ilimfanya Joshua kuendelea kumiliki mikanda ya ubingwa wa WBA, IBF na WBO aliyokuwa ameiweka ‘rehani’ dhidi ya Povetkin.

Uwanja wa Wembley umehifadhiwa tena tayari kwa ajili ya pambano la Aprili 13 mwakani la Antony Joshua. Bondia huyo ambaye ameandika rekodi ya kushinda mapambano 22 bila kupoteza, 21 akishinda kwa KO, anatarajiwa kupambana na mshindi wa pambano kati ya Tyson Fury na Deontay Wilder.

Iran yaahidi kisasi kwa Marekani, Israel kwa shambulizi la gwaride
LIVE: Waziri Mkuu akishiriki kukinasua kivuko cha MV Nyerere Ukerewe mkoani Mwanza