Meneja mpya wa klabu ya Chelsea, Antonio Conte anapigania kumbakisha kiungo mshambuliaji kutoka nchini Ubelgiji, Eden Hazard ambaye yu njiani kuondoka klabuni hapo na kwenda kusaka mahala pengine pa kucheza soka lake kuanza msimu wa 2016-17.

Hazard, amekua akihusishwa na mipango ya kutaka kujiunga na mabingwa wa soka nchini Ufaransa PSG pamoja na klabu ya Real Madrid ya nchini Hispania kutokana na klabu yake ya Chelsea kukosa nafasi ya kushiriki michuano ya ligi ya mabingwa barani Ulaya msimu ujao.

Gazeti la L’Equipe la nchini Ufaransa limeripoti kwamba, Conte amekua akihaha kumbebeleza kiungo huyo, ili abakie Stamford Bridge kwa kisingizio cha kumuhitaji kwenye mipango yake ya kuirejeshea heshima The Blues.

Hata hivyo bado haijafahamika nini mustakabali wa mazungumzo ya wawili hao, japo fununu za Hazard za kutaka kuondoka zinaendelea kupewa nafasi kubwa katika baadhi ya vyombo vya habari vya nchini England, Ufaransa pamoja na Hispania.

Hazard hakuonyesha kiwango kizuri cha soka kwa msimu huu na mara kwa mara alikua akishindwa kujihakikishia nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza, tangu alipowasili meneja wa muda Guus Hiddink.

Thibaut Courtois Aendelea Kutikisa Kibiriti
Kinnah Phiri Atoa Sababu Za Kufungwa Na Young Africans