Kiungo kutoka nchini Ufaransa Steven N’Zonzi ameutaka uongozi wa klabu ya Sevilla kukubali kumuachia katika kipindi hiki cha usajili wa kuelekea msimu mpya wa 2018/19.

Nzonzi ambaye kwa sasa yupo nchini Urusi sambamba na kikosi cha timu ya taifa ya Ufaransa, amewasilisha ombi hilo, huku akitambua meneja wake wa zamani Unai Emery ambaye amekabidhiwa kikosi cha Arsenal, amemuweka kwenye orodha ya wachezaji anaowania kuwasajili.

Hata hivyo tayari Arsenal wameshajipanga kuwasilisha ofa ya Pauni milioni 35, kwa ajili ya kiungo huyo mwenye umri wa miaka 29, ambaye bado ana mkataba wa mwaka mmoja na klabu ya Sevilla.

Lakini pamoja na harakati hizo za Arsenal kupewa nafasi kubwa, huenda klabu hiyo ya jijini London ikapata ushindani mkubwa wa kumsajili kiungo huyo, kufuatia mabingwa wa soka nchini Italia Juventus, kuripotiwa kuwa kwenye hatua za kuhitaji huduma ya N’Zonzi kwa msimu ujao.

Mchezaji huyo alijiunga na klabu ya Sevilla miaka mitatu iliyopita akitokea Stoke City ya nchini England, baada ya kugoma kusaini mkataba mpya.

Baada ya kutwaa ubingwa wa Europa League mwaka 2016, N’Zonzi alikaribia kuondoka klabuni hapo, kufuatia maelewano hafifu yaliyokuwepo kati yake na meneja wa Los Rojiblancos kwa wakati huo Eduardo Berizzo.

Purukushani za wawili hao zilikoma, baada ya kuondoka kwa meneja huyo, na uongozi wa Sevilla uahidi kumpa ruhusa N’Zonzi, endapo watapata mbadala wake, na ndipo alipokubali kusiani mkataba wa mwaka mmoja mwanzoni mwa mwaka huu.

Riyad Mahrez kuweka rekodi Leicester City
Pweza mtabiri wa kombe la dunia ageuka kitoweo Japan