Kiungo kutoka nchini Wales Aaron Ramsey, amesema bado hajaanza mazungumzo ya kusaini mkataba mpya na klabu ya Arsenal, licha ya mkataba wa sasa kutarajia kufikia kikomo mwishoni mwa msimu wa 2017/18, ambao utaanza mwezi ujao.

Kiungo huyo alijiunga na Arsenal mwaka 2008, akitokea Cardiff City FC, amesema suala la mazungumzo ya kusaini mkataba mpya, lipo chini ya uongozi wa klabu ya Arsenal, na utakapowadia muda wa kufanya hivyo hatokua na hiyana.

“Tutaangalia nini kitatokea siku za usoni, lakini nipo tayari kuendelea kuitumikia klabu hii, wakala wangu anaendelea na taratibu za kuhakikisha mazungumzo baina yangu na uongozi yanafanyika kwa wakati,” Alisema Ramsey alipohojiwa na kituo cha televisheni cha Sky Sports.

“Sina uhakika ni lini mazungumzo yataanza, lakini kwa sasa jukumu langu ni kucheza mpira na kuheshimu mkataba uliopo.”

Kwa upande wa meneja wa Arsenal Unai Emery amesema, kiungo huyo mwenye umri wa miaka 27, ana umuhimu mkubwa katika kikosi chake, na klabu inaandaa utaratibu wa mazungumzo kabla ya kumsainisha mkataba mpya.

Ramsey anatarajiwa kuwa sehemu ya kikosi cha Arsenal, katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Atletico Madrid utakaochezwa baadae nchini Singapore.

Mchezo huo wa kirafiki ni sehemu ya michuano ya kombe la mabingwa (Champions Cup) inayoendelea katika kipindi hiki cha maandalizi ya msimu mpya wa 2017/18.

Muna Love awapa moyo wanaopitia magumu
Tunakagua Leseni sio vyeti- Kamanda Muslim