Kiungo wa mabingwa wa soka nchini Ujerumani FC Bayern Munich Arturo Vidal, atakosa mchezo wa nusu fainali ligi ya mabingwa barani Ulaya dhidi ya mabingwa watetezi Real Madrid, baada ya kufanyiwa upasuaji kwa mafanikio makubwa.

Kiungo huyo alipatwa na majeraha ya goti alipokua mazoezini jana, na amelazimika kufanyiwa upasuaji, baada ya majibu ya vipimo alivyofanyiwa kuonyesha kulikua na haja ya kufanyiwa hivyo ili awahi kupona kwa wakati.

Mbali na kuukosa mchezo wa nusu fainali, ligi ya mabingwa barani Ulaya, pia Vidal hatocheza michezo ya ligi ya Ujerumani iliyosalia kwa msimu huu.

Kiungo huyo kutoka nchini Chile, hakuwahi kucheza soka tangu alipopatwa na majeraha katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa robo fainali ligi ya mabingwa barani Ulaya dhidi ya Sevilla CF uliochezwa Aprili 03, na alitarajiwa kurejea uwanjani hii leo katika mpambano wa kombe la Ujerumani dhidi ya Bayer Leverkusen, lakini kwa bahati mbaya aliumia tena akiwa mazoezini.

“Vidal amefanyiwa upasuaji, na hatua hiyo imekamilika kwa mfanikio makubwa, hatoweza kucheza tena msimu huu.” Imeeleza taarifa ya Bayern Munich.

Vidal hakumaliza mchezo wa robo fainali ligi ya mabingwa barani Ulaya dhidi ya Real Madrid msimu uliopita, baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu, ambapo katika mpambano huo Real waliibuka na ushindi wa mabao 4-2, na kusonga mbele kwa jumla wa mabao 6-3.

Msimu huu miamba hiyo imepangwa kukutana tena katika hatua ya nusu fainali, na mashabiki wengi duniani wanasubiri kuona kama Bayern Munich watalipiza kisasi chini ya meneja Jupp Heynckes.

Mchezo wa mkondo wa kwanza utachezwa April 25 mjini Munich, na Mei Mosi miamba hiyo itacheza mpambano wa mkondo wa pili kwenye uwanja wa Santiago Bernabeu, mjini Madrid.

Magazeti ya Tanzania leo Aprili 18, 2018
Burundi yatuhumiwa kwa kuminya uhuru wa wapinzani