Uongozi wa klabu ya AS Monaco umewaomba radhi mashabiki na kuahidi kurejesha fedha za vingilio walizotumia katika mchezo wao  wa jana dhidi ya PSG, ambao waliwashushia mvua ya magoli.

AS Monaco walikua na matumaini makubwa ya kuendelea kutetea taji lao, kwa kuizuia PSG wasifanye hivyo kupitia mchezo huo, lakini hali haikua nzuri, kufuatia madhila yaliyowakuta ndani ya dakika 90, jambo ambalo limewafadhaisha mashabiki wao.

Mashabiki lukuki wa klabu hiyo ya mjini Monaco, Ufaransa, walijitokeza uwanjani usiku wa jana kushuhudia ndoto hiyo ikitimia, lakini waliondoka vichwa chini baada ya kikosi chao kukubali bakora saba kwa moja.

Taarifa iliyotolewa na uongozi wa AS Monaco imeeleza kuwa, ilikua kama bahati mbaya na sio kusudio lao kupata walichokipata, lakini imewasihi mashabiki kuwa na uvumilivu na kuangalia msimu ujao.

Taarifa hiyo imeendelea kueleza kwamba, msimu ujao uongozi wa AS Monaco utahakikisha unafanya usajili wa wachezaji wenye viwango ili kurejesha heshima ya klabu ambayo kwa sasa inapigania kumaliza katika nafasi ya pili.

Mwisho taarifa hiyo ikawathibitishia mashabiki wa AS Monaco kurudishiwa fedha za viingilio.

Endapo AS Monaco wangeshinda mchezo wa jana, wangeendelea kuwa sehemu ya kupigania taji lao walilolitwaa msimu uliopita, ila kufungwa kwao wameifanya PSG kufikisha alama 87 na wao kusalia na alama 70.

Kimahesabu wawili hao wamesaliwa na michezo mitano na PSG ameshatangaza ubingwa kutokana na kuwa na idadi kubwa ya alama ambazo haziwezi kufikiwa na AS Monaco.

Pep Guardiola afikisha taji la 24, Man City 7
Makamu wa Rais atua London kumuwakilisha Rais JPM