SERIKALI imeanza kupokea maoni na ushauri kutoka kwa asasi za kiraia, sekta binafsi na wananchi kuhusu maboresho ya rasimu wa mpango kazi wa kitaifa wa uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa uwazi wa Awamu ya tano (2016/17 -2017/18).
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari leo Jijini Dar es Salaam na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya utumishi wa Umma, Susan Mlawi ilisema mwisho wa kuwasilisha maoni na ushauri huo ni tarehe 10 Septemba mwaka huu saa 9:30 alasiri.
Mlawi alisema mpango kazi huo utahusisha vipaumbele katika maeneo saba ambayo ni pamoja na upataji taarifa, takwimu huria, bajeti za wazi, uwazi kuhusu ardhi, uwazi kuhusu tasnia ya uziduaji, uwazi katika masuala ya afya, na mifumo ya utendaji kazi.
Aidha aliongeza kuwa maoni, ushauri na mapendekezo hayo yanaweza kuwasilisha Serikalini katika njia mbalimbali za mawasiliano ikiwemo tovuti rasmi ya wananchi (www.wananchi.go.tz), tovuti ya ogp (www.opengov.go.tz), government open data portal (www.opendata.go.tz).
Mlawi alizitaja njia nyingine za kuwasilisha maoni hayo ni katika barua pepe ya Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma (ps@utumishi.go.tz ) pamoja na njia ya barua kupitia sanduku la posta 2483 Dar es Salaam.
 Kwa mujibu wa Mlawi alisema rasimu ya mpango kazi inapatikana katika tovuti ya wananchi (www.wananchi.go.tz), tovuti ya ogp (www.opengov.go.tz), government open data portal (www.opendata.go.tz), tovuti ya ofisi ya Rais, menejimenti ya utumishi wa umma (www.utumishi.go.tz), pamoja na mitandao ya kijamii ya facebook (utumishi week) na blog (http://utumishiweek.blogspot.com).
“Moja ya vigezo na matakwa ya utekelezaji wa mpango huu kwa nchi mwanachama ni kuandaa mpango kazi wa kitaifa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali zikiwemo Asasi za kiraia, sekta binafsi na wananchi, hivyo Serikali inawahimiza wadau kushiriki kikamilifu kutoa maoni yao” alisema Mlawi.
Mpango wa uendeshaji wa Serikali kwa uwazi ni jitihada za kimataifa katika kuhimiza uendeshaji wa Serikali kwa uwazi zaidi, ushirikishwaji mkubwa wa wananchi, kudhibiti rushwa katika jamii na kuimarisha utoaji huduma bora kwa wananchi. Tanzania ilijiunga na mpango huo mwaka 2012.

Vijana Watakiwa Kutobweteka
Video: Waziri Maghembe apokea msaada wa magari 10 kutoka Frankfurt Zoological Society