Naibu Waziri wa mambo ya ndani Hamad Masauni amemuagiza Kamanda wa kikosi cha usalama barabarani kuwakamata Askari walioonekana wakimtukana na kumpiga vibao dereva mmoja kwenye gari la mizigo.

Jana mitandaoni kumekusambaa video ikionesha askari mmoja akimchapa makofi na kumtukana dereva wa gari la mizigo, huku akisikia akimwambia anaomba leseni yake na kuwataka waliopanda kwenye gari hilo kulala chini

Ambapo wananchi mbalimbali wametoa maoni wakimtaka askari huyo kuchukuliwa hatua za kisheria kwa kosa la kujichukulia sheria mkononi ya kumuadhibu kwa kipigo na matusi dereva huyo.

Masauni leo amezungumza na vyombo vya habari akithibitisha kuwa tayari askari huyo na wenzake waliohusika na tukio hilo wametiwa mbaroni kusubiria taratibu nyingine za kisheria.

”Nimeshawaelekeza jeshi la polisi hususani kamanda usalama barabarani kuhakikisha anachukua hatua kali dhidi ya wale wahusika, hiyo taarifa nimepata jana usiku wakati huo huo nilimjulisha na ameshaniarifu kwamba askari hao wapo kizuizini mpaka taratibu rasmi za mashtaka zitapofunguliwa dhidi yao” Masauni.

Aidha kumekuwa na maoni mbalimbali kutoka kwa wananchi kufuatia tukio hilo wakidai kuwa imekuwa tabia ya askari wengi wa barabarani kuwadhalilisha na kuwanyanyasa madereva huku wakisahau kuwa madereva hao wameacha familia majumbani kwao.

Kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram mwananchi mmoja anayeenda kwa jina la coxdawayao amesesma.

”Hao askari huwa wanasahau sisi madereva tuna wake na watoto majumbani utakuta askari ana miaka 19 anamtukana dereva wa miaka 45”.

Hivyo wananchi wameomba tabia hiyo ikomeshwe dhidi ya maaskari wanaojichukulia sheria mkononi kwani kwa sasa imekithiri.

 

Polisi Kagera waua majambazi watatu
Maalim Seif atangaza kuhamia ACT- Wazalendo baada ya uamuzi huu wa Mahakama