Kitendawili cha chanzo cha uhasama unaosadikika kuwepo kati ya mafahari wawili wa Bongo Fleva, Diamond na Ali Kiba kimewashinda wengi, na sasa mwimbaji AT ameamua kuvunja nazi hadharani kueleza kilichojili.

AT amedai kuwa wawili hao waliokuwa karibu miaka kadhaa iliyopita, walijikuta wakitaka kurushiana makonde Oman, katika chumba chake cha hotel ambayo wote walikuwa wamefikia kwa ajili ya kufanya tamasha, na kwamba yeye ndiye aliyeamua ungomvi huo.

Akifunguka kupitia kipindi cha Shilawadu cha Clouds TV, AT alisema kuwa wawili hao walikuwa wakicheza game ndani ya chumba chake lakini kabla hawajafika mbali walipishana kauli, ambapo Ali Kiba aliamka na kumpa onyo Diamond akieleza kwa hasira historia ya ugomvi wao.

“Ali Kiba alitaka kuzirusha za Tyson pale, mimi ndiye nilikuwa katikati yao. Alisimama akamwambia halafu wewe nimekuwa nikikuangalia ulishafanya hili, hili, hili na lilee,” alisema AT huku akiweka sharti kuwa ataeleza undani wa chanzo hicho hivi karibuni endapo wawili hao hawatafunguka.

“Yaani hadi leo tungekuwa na msanii mmoja ama ni chongo ama ni pengo kama yangeharibika siku ile,” aliongeza.

Hata hivyo, anadai alifanikiwa kusuluhisha ugonvi huo kwa siku hiyo lakini aligundua ugomvi huo ulikuwa na mengi nyuma ya pazia.

Alidai kuwa hata waandaaji wa show hiyo walikuwa na maswali mengi kuhusu mafahari hao kwani hawakutaka kupanda ndege moja wala kushare maeneo kadhaa kwa kipindi fulani.

Ikumbukwe kuwa AT ameturudisha nyuma zaidi ya matukio yaliyokuwa yakitajwa, hasa pale Ommy Dimpoz alipowahi kueleza kuwa Diamond aliondoa vionjo vya Ali Kiba kwenye wimbo wake wa ‘Lala Salama’, na Ali Kiba kumuondoa Diamond kwenye ‘Single Boy’.

Roma aeleza kwanini alifundisha Mchikichini, sasa ana ‘Bodyguard’
Video: Lowassa alitingisha tena Bunge Dodoma, Wabunge wataka maandamano