Naibu Waziri wa Maji ,Jumaa Aweso ameahidi kuwa wizara yake itawalipa wakandarasi wa miradi ya maji inayofadhiliwa na benki ya dunia katika wilaya ya Ngara mkoani Kagera kiasi cha Sh 433.46 milioni baada ya kucheleweshewa fedha hizo kutoka serikalini tangu mwaka 2014.

Ameyasema hayo katika ziara ya siku moja wilayani Ngara baada ya kupokea taarifa kutoka kwa kaimu mhandisi wa maji wa halmashauri ya wilaya ya Ngara Simon Ndyamukama aliyesema wananchi wanapata maji kwa asilimia 63.

Pia ameagiza wahandisi na wakandarasi ambao miradi yao imeonekana kuwa na changamoto za utekelezaji pamoja na wahandisi wa halmashauri za wilaya ya Muleba na Misenyi kufika ofisini kwake mkoani Dodoma kujieleza kabla ya kuchukuliwa hatua za kisheria

Amesema kuwa wahandisi wa halamshauri hizo za Misenyi na Muleba wamelalamikiwa kwa kulipa fedha za miradi ya maji lakini haijakamilika na miradi mingine inavuja matenki au mabomba na kwamba mhandisi wa Ngara ameonekana kufanya kazi kwa uadilifu na uaminifu.

“Atakayeshirikiana na wakandarasi kutafuna fedha za serikali za miradi ya maji kila halmashauari nchini atazitapika na sisi watendaji wa wizara tutamchukulia hatua za kisheria na wala hatutamuhamisha ahtawajibishwa kwenye kituo chake cha kazi,”amesema Aweso.

Aidha, amesema kuwa ameridhishwa na utekelezaji wa miradi ya maji katika vijiji 10 wilayani Ngara na kushauri baraza la Madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo kumthibitisha kaimu mhandisi wa maji Simon Ndyamukama kushikilia ofisi na kutimiza majukumu yake ipasavyo.

Hata hivyo, katika taarifa aliyosomewa kuhusu upatikanaji wa maji wilayani humo,amelazimika kutembelea mradi wa maji Muhweza utakaogharimu Sh. 559.4 milioni ambao umetekelezwa kwa asilimia 80 licha ya kuwepo changamoto ya ucheleweshaji wa fedha toka serikali tangu 2014.

 

Video: Lugola atoa agizo trafiki kupigana na dereva Songwe, Lissu aanza ziara Ulaya
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Januari 14, 2019