Watu watatu wameuawa kwa risasi baada ya mshambuliaji kufyatua risasi katika hospitali ya Chicago nchini Marekani, na baadaye kujiua.

Kwa mujibu wa msemaji wa polisi, mshambuliaji huyo alianza mashambulizi akimlenga zaidi mwanamke aliyewahi kuwa mpenzi wake.

Ripoti za awali zimeeleza kuwa mshambuliaji huyo aliuawa, ingawa taarifa nyingine zinadai alijipiga risasi. Hivyo, polisi wamesema watatoa taarifa ya uhakika juu ya kifo cha mshambuliaji huyo na utambulisho wake.

Madaktari wawili wa kike ni miongoni mwa watu walioua, kwa mujibu wa Meya Rahma Emanuel. Mwingine aliyeuawa ni askari polisi aliyekuwa anajaribu kumdhibiti mshambuliaji huyo.

“Mshambuliaji alifyatua risasi kadhaa akianzia katika eneo la kuegesha magari la hospitali, na alidhibitiwa wakati anazidi kujaribu kuelekea ndani ya jengo,” Msemaji wa Idara ya Polisi ya Chicago anakaririwa.

Vipande vya video vilivyowekwa mitandaoni vilionesha watu wakikimbia kunusuru maisha yao wakiwemo wafanyakazi wa hospitali hiyo walikuwa wamevalia sare.

Hata hivyo, uongozi wa hospitali hiyo ulitoa tangazo baadaye kuwa wamefanikiwa kudhibiti hali hiyo na shughuli zimerejea katika hali ya kawaida.

Takribani watu 13,000 wameuawa kwa risasi mwaka huu nchini Marekani kwa mujibu wa mtandao maalum wa Gun Violence Archive. Imeelezwa kuwa watu 25,000 walijeruhiwa. Pia, takwimu hizo zinaonesha kuwa askari polisi 250 walipigwa risasi wakiwa kazini.

Wanafunzi wanaswa na simu kwenye chumba cha mtihani
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Novemba 20, 2018