Matajiri wa Dar es salaam Azam FC, wana mechi mbili za moto kukamilisha mzunguko mzima wa Ligi Kuu Bara msimu wa 2022/23.

Awali mechi hizo mbili zilitarajiwa kuchezwa Mei 24 na 28, mwaka huu, lakini kwa sasa zimesogezwa mbele hadi Juni 6 na 9, 2023.

Azam FC itaanza dhidi ya Coastal Union, mechi itakayopigwa Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, itakuwa Juni 6, kisha kete yao ya mwisho dhidi ya Polisi Tanzania, Juni 9, 2023.

Kwenye mechi hizo mbili, moja watakuwa ugenini dhidi ya Coastal Union ambayo kwenye mzunguko wa kwanza iliibuka na ushindi wa mabao 3-2 na kete ya pili watakuwa nyumbani dhidi ya Polisi Tanzania ambao kwenye mzunguko wa kwanza walishinda bao 1-0 ugenini.

Ugumu upo kwenye mechi hizo kutokana na timu zote kusaka alama tatu, Coastal Union inapiga hesabu za kulipa kisasi cha kufungwa nyumbani ikiwa na pointi 33 nafasi ya 10, huku Polisi Tanzania ikipambana kutoshuka daraja ikiwa nafasi ya 15 na alama 25.

Kali Ongala, Kocha wa Azam FC, amesema wanatambua umuhimu wa mechi zilizobaki, hivyo watafanya jitihada kupata pointi tatu.

“Tunatambua umuhimu wa mechi ambazo zimebaki, tutafanya maandalizi muhimu kupata pointi zote sita,” amesema

Usiyoyajua kuhusu malipo ya Bima ajali vyombo vya moto
Mwanapatholojia wa Serikali kuongoza zoezi upasuaji maiti 128