Klabu ya Azam FC, imemtoa kwa mkopo mshambuliaji wao, Tape Edinho, kwenda Klabu ya Stella Club d’Adjame ya Ivory Coast kuitumikia kwa kipindi cha miezi sita.

Edinho aliyesajiliwa kwa mkataba wa miaka miwili na Azam FC katika usajili wa dirisha kubwa, ametolewa kwa mkopo ili kutoa nafasi kwa kipa raia wa Ghana, Abdulai Iddrisu, aliyejiunga na klabu hiyo katika kipindi cha dirisha dogo kwa ajili ya kukiimarisha timu hiyo katika michezo iliyopo mbele yao, Ligi Kuu Tanzania Bara na Kombe la Shirikisho (FA Cup).

Afisa Habari wa Azam FC, Thabiti Zakaria ‘Zaka Zakazi’, amesema kwa sababu ya Kanuni ya Shirikisho la Soka nchini (TFF), kila klabu kutakiwa kusajili idadi ya wachezaji wakigeni wasiozidi 12, wameamua kumtoa Edinho kwa mkopo ili kumpa nafasi kipa huyo.

Amesema kwa kuzidi mchezaji mmoja wanalazimika kumtoa kwa mkopo mshambuliaji huyo kwenda nyumbani kwao kuitumikia Stella Club d’Adjame.

“Tukumbuke dirisha dogo tumesajili kipa kutoka nchini Ghana (Iddrisu), uwapo wa nyanda huyo unafanya timu yetu wachezaji wa kigeni kuwa 13, lazima mmoja aondoke twende sawa na Kanuni ya TFF, tumemtoa kwa mkopo Tape kwa muda wa miezi sita baadae atarejea katika klabu yake ya Azam FC,” amesema Zakazi.

Amesema wamelazimika kufanya usajili wa kipa na kupunguza mchezaji wa ndani kwa sababu nafasi walioongeza mtu ilikuwa na shida na wanaimani kipa huyo atasaidia timu hiyo kufikia malengo yake.

Zakazi amesema matarajio yao makubwa ni kuhakikisha wanamaliza nafasi tatu za juu katika ligi pamoja na kufanya vizuri katika Kombe la FA kwa kufuzu hatua ya 32 na kutwaa taji hilo.

Azam FC kwa sasa ipo nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara ikiwa na alama 43, saba nyuma ya Simba iliyoko nafasi ya pili na 10 nyuma ya vinara wa ligi hiyo, Young Africans.

Polisi, Wananchi wafukua kaburi kupata ukweli
Frank Lampard akalia kuti kavu Everton