Kampuni ya Azam Media Limited leo imesaini Mkataba wa miaka minne na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa ajili ya kudhamini michuano ya Kombe la Shirikisho, zamani (FA) wenye thamani ya Sh. Bilioni 3.3.

Katika halfa iloyofanyika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa jengo la Kisenga LAPF, Kijitonyama, Dar es Salaam, Rais wa TFF, Jamal Malinzi, amesema kwamba amefurahia kufanikisha azma ya kurejesha mashindano hayo.

Malinzi amesema kwamba duniani kote maendeleo ya soka yanatokana na kuwepo na mashindano mbalimbali yakiwemo ya Kombe la Shirikisho la nchi, ambayo yanashirikisha na klabu za chini hadi zile zinazoshiriki Ligi Kuu.

“Nitafurahi sana kuona klabu ya Daraja la Pili inashinda Kombe hilo, duniani kote Kombe hili lipo na klabu za chini zimekuwa zikiwapiga ‘visu’ wale wakubwa,” alisema Malinzi.

Aliongeza kuwa bingwa wa mashindano hayo atajinyakulia kitita cha Sh. Milioni 50 wakati kila timu itakayokwenda kucheza ugenini itapata Sh. Milioni tatu za safari na mwenyejii atapewa Sh. Milioni 1 ya maandalizi.

“Tumeona bingwa wa michuano hii apate Sh. Milioni 50 kwa sababu atakuwa amecheza mechi saba na yule wa Vodacom anayecheza michezo 30 anapata Sh. Milioni 70,” Malinzi aliongeza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya TFF, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’ alisema jana kuwa mashindano ya mwaka huu yatashirikisha klabu 64 na yataendeshwa kwa njia ya mtoano.

Kaburu, ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Simba SC, amezitaja timu hizo kuwa ni pamoja klabu 16 zinazoshiriki Ligi Kuu ya Bara, timu 24 za Daraja la Kwanza na idadi kama hiyo za Daraja la Pili.

Alisema kwamba mshindi wa kombe hilo atapata nafasi ya kuiwakilisha nchi katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika (CAF) mwaka 2017.

Alieleza kuwa timu 16 za Ligi Kuu ya Bara zenyewe zitaanzia raundi ya pili itakayoshirikisha klabu 32 na kuongeza kwamba wiki ya mechi za Kombe la FA hakutakuwa na michezo ya Ligi ya Bara.

Hii ni mara ya kwanza kihistoria michuano ya Kombe la FA kuwa na udhamini na miaka ya imekuwa ikiibuka na ‘kuyeyuka’ tangu mwaka 1967 kabla ya kupotea moja kwa moja mwaka 2002.

Mara ya mwisho Kombe la FA lilifanyika mwaka 2002 na JKT Ruvu Stars ya Pwani ikaibuka bingwa baada ya kuifunga Baker Rangers ya Magomeni kwenye fainali.

Bingwa wa kwanza wa Kombe la FA enzi hizo likiitwa Kombe la FAT ilikuwa Yanga SC mwaka 1967, na michuano hiyo haikufanyika tena hadi 1985 Maji Maji ya Songea ilipotwaa Kombe.

Kombe la FAT likayeyua tena kabla ya kurejea miaka 10 baadaye, 1995 na Simba SC ikatwaa ubingwa kabla ya kupokonywa na Sigara mwaka 1996, ambao nao walilitema kwa Tanzania Stars mwaka 1997 iliyofanikiwa kulitetea 1998 kabla ya kupokonywa na Yanga SC 1999.

Ubingwa wa FA mwaka 2000 ulikwenda kwa  Simba SC, waliopokonywa na Yanga SC mwaka 2001 kabla ya JKT Ruvu kuwa bingwa wa mwisho wa mashindano hayo mwaka 2002.

FA Wahuzunishwa Na Adhabu Ya Eva Carneiro
Van Gaal Kumrejesha Kundini De Gea