Baba mzazi wa watoto watatu Cosmas Chacha (45) anayeishi  Kivule jijini Dar es Salaam, amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu akikabiliwa na mashitaka ya kuwakeketa  watoto wake wenye umri chini ya miaka 18 na kuwasabibishia maumivu makali sehemu zao za siri.

Mshtakiwa Chacha amefikishwa mahakamani hapo Jumatatu Januari 6, 2019 na kusomewa mashitaka matatu mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Rashidi Chaungu.

Akisoma mashitaka Wakili wa Serikali Faraji Nguka amedai, Desemba 8, 2019 huko katika eneo la Kivule jijini Dar es Salaam, mshtakiwa Chacha akiwa baba mzazi na mwenye jukumu la kuwalea mabinti hao watatu (majina yamehifadhiwa) aliwapeleka kufanyiwa ukeketaji hali iliyowasababishia maumivu makali sehemu zao za siri na majeraha.

Hata hivyo, mshtakiwa amekana kutenda makosa hayo na amerudishwa rumande baada ya kushindwa kutimiza Masharti ya dhamanana yaliyomtaka kuwa na wadhamini wawili mwenye barua na vitambulisho watakaosaini bondi Sh.Milioni tano.

Kwa mujibu wa upande wa mashtaka upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika na kesi hiyo itatajwa tena mahakamani hapo Januari 20 mwaka huu.

Madhehebu ya dini kupigwa kitanzi Mbeya, RC Chalamila atangaza uhakiki
RC Chalamila apiga marufuku matangazo ya waganga wa jadi