Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Simba SC, wameendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu Soka Tanzania Bara kwa kufikisha alama 73, na kuiacha Young Africans yenye alama 67.

Mavuno ya alama tatu kwa mabingwa hao wa Tanzania Bara yametoka kwenye timu ya Mbeya FC iliyogunga safari kutoka jijini Mbeya, baada ya kuichabanga mabao 4-1, Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam.

Dakika 90 za mchezo huo zimeshuhudia Simba SC ikimaliza dakika 45 za kipindi cha kwanza ikiongoza mabao mawili yaliofungwa na viungo Larry Bwalya na Luis Miquissone.

Kipindi cha pili Nahodha na Mshambuliaji wa Simba SC John Bocco aliongeza bao la tatu kabla ya kiungo Clatous Chama hajaongeza bao la nne. Bao la kufutia machozi la Mbeya City FC limefungwa na Pastory Athanas.

Simba SC yenye michezo miwili mkononi mkononi tofauti na Young Africans, inahitaji alama tatu nyingine kujihakikishia Ubingwa wa Tanzania Bara kwa mara ya nne mfululizo.

Mchezo ujao kwa mabingwa hao utawakutanisha dhidi ya Young Africans,  mnamo Julai 03 Uwanja wa Benjamin Mkapa,  Dar es salaam, baada ya mchezo wa Mei 08 kuahirishwa kufuatia sababu zilizokua nje ya uwezo wa mamlaka za soka nchini Tanzania.

Hata hivyo miamba hiyo itapapatuana baada ya michezo ya Nusu Fainali ya Kombe la Shirikisho (ASFC),  itakayochezwa mwishoni mwa juma hili.

Young Africans watapambana dhidi ya Biashara United Mara, Uwanja wa Ally Hassan Mwinyi Mjini Tabora, Ijumaa (Juni 25).

Simba SC ambayo ni Bingwa Mtetezi wa ASFC itapapatuana dhidi Azam FC, mjini Songea mkoani Ruvuma kwenye Uwanja wa CCM Majimaji, Jumamosi (Juni 26).

Rais Samia afanya mabadiliko uteuzi Wakuu wa Wilaya
DPP awaachia huru watuhumiwa 14