Baada ya timu ya Tanzania Bara Kilimanjaro Stars kupoteza mchezo dhidi ya Zanzibar Heroes  kwenye michuano ya Cecafa Senior Challenge inayoendelea hapa nchini Kenya Kocha Mkuu wa kikosi hicho, Ammy Ninje amesema kikosi chake bado kina nafasi ya kufanya vizuri kwenye mechi mbili zilizobaki.

Kilimanjaro Stars iliyopo katika kundi A imebaki na michezo dhidi ya Rwanda na wenyeji Kenya ambayo Kocha Ninje anaamini watashinda na kusogea hatua ya nusu fainali.

Akizungumzia Kilimanjaro kupoteza mchezo dhidi ya Zanzibar, Kocha Ninje amesema kipindi cha kwanza timu ilicheza vizuri kiasi cha kupata goli lililofungwa na nahodha Himid Mao, lakini kipindi cha pili wakaanza taratibu na kuwaruhusu Zanzibar kurudi mchezoni hali iliyopelekea ushindi wao.

Amesema makosa mawili yaliyofanyika ndio yamewaghalimu kupoteza lakini kimpira timu imecheza mchezo mzuri.

“Kuliko kuangalia makosa ya mchezaji mmoja mmoja Nimewaambia Wachezaji wangu wasikate tamaa bado tuna nafasi ya kufanya vizuri katika mechi zetu mbili zilizobaki,” amesema Ninje.

Kwa matokeo hayo Kilimanjaro Stars inabakiwa na pointi 1 baada ya kucheza michezo miwili katika kundi hilo la A ikisaliwa na michezo dhidi ya Rwanda “Amavubi” na wenyeji Kenya ‘Harambee Stars’.

Harmonize, Sarah uso kwa uso na Wolper usiku wa leo
Kilimanjaro Stars yaufyata kwa Z,bar Heroes