Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amemteua balozi John Kijazi kuwa mwenyekiti wa bodi ya ushauri ya wakala wa ndege za Serikali (TGFA).

Wakati huo huo amemteua mhandisi Frolian Kabaka kuwa mwenyekiti wa bodi ya ushauri ya wakala wa barabara vijijini na mijini (TARURA).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kitengo cha habari Ikulu, uteuzi huo umeanza februari 26, 2020.

Balozi kijazi pia ni Katibu mkuu kiongozi , na aliwahi kuwa mwakilishi wa Tanzania nchini India, Singapore, Sri Lanka, Bangladesh na Nepal mwenye makazi yake jijini New Delhi, India kuanzia mwaka 2007 na hivyo kumfanya kuwa Mkuu wa Mabalozi wote wanaowakilisha Tanzania nje ya nchi.

Mhandisi Kijazi alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na baadaye Wizara ya Maendeleo ya Miundombinu kuanzia mwaka 2002 hadi 2006, baada ya kuteuliwa kuwa Balozi ndani ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na hatimaye kupangiwa kituo cha New Delhi, India.

Kati ya mwaka 1996 hadi 2002, Kijazi alikuwa Mhandisi Mwandamizi wa Ujenzi wa Barabara ndani ya Wizara ya Ujenzi kabla ya kupandishwa cheo na kuwa Mkurugenzi wa Barabara za Mikoa ndani ya Wizara hiyo hiyo.

Balozi Mhandisi Kijazi alipata Shahada ya Sayansi ya Uhandisi wa Umma mwaka 1982 kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam, na baadaye Shahada ya Uzamili katika Uhandisi wa Barabara Kuu kutoka Chuo Kikuu cha Birmingham, Uingereza mwaka 1992.

Henga: watumishi wa LHRC wanapewa vitisho
Utaratibu mpya kumpata Miss Tanzania watangazwa