Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) limetangaza utaratibu mpya wa kidijitali wa kupokea na kukagua nyimbo za wasanii kwa kutumia WhatsApp ili kuendana na kasi ya utoaji wa nyimbo.

Katibu Mtendaji wa Baraza hilo, Godfrey Mngereza amesema kuwa utaratibu huo umenzishwa kwa lengo la kuwaondolea usumbufu wasanii ambao baadhi yao wako mikoani, kufika katika ofisi za Baraza kuwasilisha kazi zao na kusubiri majibu.

“Teknolojia imekuwa kubwa, hatuoni tena sababu ya kumsumbua msanii aje ofisi kwetu kwa ajili ya kukaguliwa nyimbo wakati kazi hiyo anaweza kuifanya hata akiwa nyumbani kwake,” Mngereza anakaririwa.

“Pia, tunaamini itampunguzia gharama na kuokoa muda ambao atautumia kufanya mambo mengine, hivyo wale waliokuwa na visingizio ya hayo sasa hatufikirii tena kuvisikia kwani tumewarahisishia maisha ni wao wenyewe,” ameongeza.

Amezitaja namba zinazotumika kupokea nyimbo hizo na kutoa majibu kuwa ni 0783 965 337, ambapo amesema majibu hayo yatatolewa haraka.

Kwa mujibu wa sheria, kazi za wasanii zinapaswa kuwasilishwa katika baraza hilo kwa ajili ya kukaguliwa na kupata ruhusa kabla ya kutolewa kwa ajili ya umma.

Antonio Conte anukia Santiago Bernabéu
Ripoti: Hakuna ‘makazi duni’ Tanzania, ni mpangilio