Wanafunzi 51 nchini Italia waliokuwa kwenye gari la shule wamenusurika kifo baada ya gari lao kutekwa na kisha kuteketezwa kwa moto wakiwa ndani, huku dereva wa gari hilo akisherehekea kitendo hicho.

Wanafunzi hao wa shule ya Vailati di Crema iliyo karibu na jiji la Milan walikuwa na walimu wao wakielekea kwenye mazoezi, lakini dereva wa gari hilo alibadili muelekeo ghafla na kulielekeza kwenye njia inayoelekea Uwanja wa Ndege wa Milan Linate siku ya jana, kwa mujibu wa BBC.

Walimu waliokuwa kwenye gari hilo wameeleza kuwa dereva huyo alisikika akishangilia na kupaza sauti akijinadi, “hakuna hata mmoja atakayenusurika.”

Mwalimu mmoja amekaririwa akidai kuwa dereva alikuwa na tabia ya hasira na kufoka mara kadhaa hapo awali, na kwamba katika tukio hilo alitoa matamshi makali wakati watekaji wakilichoma moto basi hilo.

Dereva huyo mwenye umri wa miaka arobaini anadaiwa kusimama na kuwaelekezea kisu abiria wake na kutoa maneno ya vitisho ikiwa ni pamoja na maelezo yanayoilenga Serikali kuwa waache kufanya mauaji katika bahari ya Mediterranean.

Hata hivyo, wakati akifoka na kutoa vitisho, mvulana mmoja aliwapigia simu wazazi wake kwa siri na wao wakawataarifu polisi waliofika kwenye eneo la tukio haraka.

Polisi wameeleza kuwa walikuta basi likiwa linawaka na limezungushiwa mafuta ya petrol lakini walifanikiwa kubomoa kioo cha nyuma na kuwatoa abiria wote na kumkamata dereva huyo.

Kwa mujibu wa taarifa ya polisi, hakuna abiria aliyejeruhiwa vibaya lakini watu 13 waliathiriwa na moshi uliotokana na kuungua kwa basi hilo.

 

 

 

Video: Chadema wampongeza Rais Magufuli, Nassari amburuta Spika Bungeni
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Machi 21, 2019