Benard Paulo Mnyang’anga aka Ben Pol siyo mtu wa hivi-hivi! Siyo yule wa ‘Number One Fan’, hivi sasa ananukia umilionea. Ndivyo unavyoweza kuanza simulizi la maisha mapya ya mkali huyu wa RnB kwa lugha ya mtaani.

Mkali huyo wa ‘Pete’ ameweka wazi kitita cha mamilioni ya shilingi aliyotumia kununua pete ya uchumba aliyomvika mpenzi wake, Anerlisa, raia wa Kenya aishie Ughaibuni.

Akizungumza kwenye mahojiano maalum aliyofanya hivi karibuni na Zamaradi Mketema, Ben Pol amesema kuwa alitumia $11,000 (zaidi ya Shilingi Milioni 22 za Kitanzania) kununua pete hiyo iliyokaa kwenye chanda chema cha Anerlisa.

Amesema mrembo huyo amekubali ombi lake la kufunga naye pingu za maisha na kwamba tangazo rasmi la tarehe na mahali vitawekwa wazi muda utakapofika.

Katika hatua nyingine, Ben Pol ameeleza kuwa ameandika historia ya kuwa msanii wa kwanza Tanzania kuingia kwenye mgahawa wa Salt Bay uliopo Dubai, Falme za Kiarabu.

Mgahawa huo hutembelewa na wasanii wakubwa duniani, wana michezo maarufu kama Lionel Messi, DJ Khalid pamoja na mamilionea kadhaa. Mgahawa huo ni moja kati ya migahawa aghali zaidi Dubai.

Wakati anaendelea kula bata, Ben Pol amepunguza kasi ya kufanya kazi ya muziki. Alipoulizwa sababu alifunguka, “dili niliyopata UN (Umoja wa Mataifa) na matamasha niliyofanya yananifanya niwe na kipato kiasi kwamba hata nisipotoa nyimbo kwa muda flani [haiumizi sana].”

Ben Pol ametengua kitendawili wanachokitega baadhi ya watu kuwa huenda fedha za bata na pete alizitoa Anerlisa. Ameeleza kuwa fedha hizo ni zake zinazotokana na matamasha mengi aliyofanya mwaka jana pamoja baadhi ya dili alizopata.

Muuguzi aliyeuwa wagonjwa 85 afungwa maisha
Monko amjibu Nyalandu, 'CCM iko imara sana'