Benki ya Dunia, imesema kuwa imekubaliana na Serikali ya Tanzania kubadili msimamo wake kuhusu elimu kwa watoto wa kike, kama sehemu ya sharti la mkopo wa $300 Milioni (Sh 680.5 bilioni).

Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia, Dkt. Hafez Ghanem amewaambia waandishi wa habari kuwa Benki hiyo bado haijatoa fedha hizo na kwamba itaendelea na mchakato wa kuziwasilisha baada ya kutekelezwa kwa makubaliano hayo.

Alisema kuwa Benki hiyo inatoa fedha kwa ajili ya maendeleo ya elimu kwa wasichana bila kujali hali yao, hivyo Serikali inapaswa kuweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha wanafunzi wanaopata ujauzito wanaendelea na masomo.

“Wataalam wetu watashirikiana na Serikali kuona ilivyojiandaa kutoa elimu kwa wasichana wote. Tutakapojiridhisha, Bodi ya Wakurugenzi itaidhinisha mkopo husika. Kuchelewa kwake kutategemea lini Serikali itatekeleza masharti tuliyokubaliana,” alisema Dkt. Ghanem.

Serikali ilieleza kuwa fedha hizo zitakazotolewa na Benki ya Dunia zitatumika katika kuboresha elimu, kwa kujenga madarasa, mabweni ya wanafunzi pamoja na nyumba za walimu.

Akizungumza jana kwenye mahojiano na BBC, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Mashariki Mashariki, Dkt. Augustine Mahiga alisema kuwa wamekubaliana na Benki hiyo kuandaa mazingira ambayo yataruhusu wanafunzi wanaopata ujauzito wanaendelea na masomo yao.

Waziri Mwakyembe aitaka Taifa Stars kutowaangusha Watanzania
Video: Makundi mawili CCM yampinga Magufuli, Mikoa hii hatari kwa wizi wa magari, Wakulima Korosho kulipwa haraka