Benki ya Dunia imetoa kiasi cha shilingi Bilioni 21.7, fedha ambazo zitatumika kuboresha miundombinu, kujenga Soko kuu la Kisasa, Kituo kikubwa cha Mabasi pamoja na Barabara za mitaa mkoani Mtwara.

Hayo yamesemwa na Afisa Mipango wa Manispaa ya Mtwara Mikindani, Ernest Mwongi wakati wa ziara ya Katibu wa CCM mkoani humo, Sadi Kusilawi ambapo amesema kuwa tangu mwezi June mwaka jana, Manispaa ya Mtwara Mikindani ilianza kutekeleza mradi wa kuendeleza miji wa  TSCP kwa awamu ya pili baada ya kupata fedha toka Benki ya Dunia zaidi ya shilingi Bilioni 21.7.

“Kiasi hicho cha shilingi Bilion 21.7 kitatumika kujenga Soko la kisasa ambalo baada ya kukamilika litakua na Ghorofa, Kituo Kikubwa cha Mabasi cha Kisasa, Barabara za Lami za Mitaa pamoja na kuweka taa za Barabarani”.Amesema Mwongi.

Aidha, kwa upande wake Mkuu wa wilaya hiyo, Evod Mmanda amesema kuwa kukamilika kwa miradi hiyo kutabadili muonekano wa Mkoa wa Mtwara ambao ni Kitovu cha Uchumi wa Mikoa ya Kanda ya kusini.

Hata hivyo, katibu huyo wa CCM amepongeza jitihada za usimamizi zinazofanywa na viongozi wa serikali na kuwataka kuendelea na kasi hiyo iliyopo ili kuhakikisha miradi yote inakamilika kwa wakati.

Ziara hiyo ya katibu wa CCM  katika Manispaa ya Mtwara Mikindani ni mwendelezo wa ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali mkoani humo ambapo msisitizo ni kuwataka wasimamizi kuzingatia makubaliano ikiwemo kukamilisha kwa wakati na kuzingatia viwango vinavyo kubalika.

Video: Malima awasha moto sakata la Diwani kukunja nne kikaoni
Wangabo atoa wiki tatu kwa Wajasiliamali Sumbawanga