Bilionea na mmiliki wa klabu ya Leicester City FC, Vichai Srivaddhanaprabha amethibitishwa kuwa miongoni mwa watu waliofariki katika ajali ya helikopta iliyotokea karibu na uwanja wa klabu hiyo siku ya Jumamosi.

Klabu hiyo pamoja na polisi wamethibitisha kuwa Vichai Srivaddhanaprabha, kutoka Thailand, wafanyakazi wake wawili, Nursara Suknamai na Kaveporn Punpare pamoja na rubani, Eric Swaffer na mpenzi wake Izabela Roza Lechowicz wamefariki dunia baada ya ndege hiyo kuanguka.

Walioshuhudia walisema waliiona ndege hiyo ikiondoka uwanjani kabla ya kupoteza mwelekeo na kudondoka kutoka angani huku wengine wakisema kuwa waliona moto mkubwa wakati ikianguka.

Maelfu ya watu wameweka maua na skafu za ukumbusho nje ya uwanja wa King Power, na pia ujumbe wa kuwafariji waliofiwa.

Kitabu cha kutoa rambirambi kitawekwa kwenye uwanja wa King Power kuanzia kesho Jumanne.

Mechi iliyokuwa inafuata ya klabu hiyo dhidi ya Southampton katika Kombe la EFL ambayo ilipangiwa kuchezwa Jumanne sasa imeahirishwa.

Leicester walikuwa wametoka sare ya bao 1-1 dhidi ya West Ham kwenye uwanja wa King Power huku mechi ikikamilika saa moja kabla ya helikopta hiyo kupaa kutoka uwanjani.

Vichai Srivaddhanaprabha mwenye umri wa miaka 60, aliinunua klabu ya Leicester kwa Euro 39 milioni mwaka 2010.

 

Mwili wa Isaac Gamba unaagwa Lugalo muda huu
Video: Diamond, Wema Sepetu, Amber Ruth wanatakiwa kuwa Gerezani - Musiba