Mgombea mwenza wa urais wa Muungano wa Kenya Kwanza, Rigathi Gachagua hatimaye amepiga kura majira ya saa 7.39 asubuhi ya leo Agosti 9, 2022, baada ya hapo awali kutotambulika kwa njia ya kibayometriki ili kupiga kura yake.

Gachagua, alilazimika kutambuliwa kupiga kura kupitia sajili ya mikono, baada ya majaribio kadhaa kupitia kitengo cha Usimamizi wa Uchaguzi Mkuu wa Kenya (KIEMs), kwa kutumia alama zake za vidole kufeli.

Kuchelewa kwa Gachagua kupiga kura, kumezua wasiwasi miongoni mwa wafuasi wake, kutokana na mgombea huyo kulazimika kusugua vidole vyake na leso, kabla ya kutambuliwa na kuruhusiwa kupiga kura, huku ikidaiwa pia mfumo wa upigaji kura pia haukuweza kutambua shangazi wa Gachagua Gladys Karaba ambaye alikuwa na matatizo ya kimwili.

Mbunge wa Mathira Rigathi Gachagua akipiga kura katika kituo cha msingi cha Sagana. kulia ni shangazi wa Gachagua, Gladys Karaba.

Akihutubia Wanahabari baada ya kupiga kura, Gachagua amesema licha ya hitilafu hiyo ya kiufundi anaamini kuwa zoezi hilo litakuwa huru, haki na la uwazi.

Mfumo wa kifurushi cha Kims, bayometriki za wapiga kura unahusisha nakishi ya vidole 10 na kidole kimoja kilichotambuliwa vyema kinachukuliwa kuwa kitambulisho chanya, ambapo ikiwa hakuna kidole kimoja kati ya 10 kitakachotambuliwa, makarani wa IEBC wanatumia utafutaji wa alpha-numeric.

Kitambulisho cha utafutaji cha alpha-numeric hutumika pale ambapo paspoti au kitambulisho cha mpiga kura huchanganuliwa, na wakati matokeo chanya yanapojitokeza, wanaombwa kuweka vidole vyao kwenye kit ili bayometriki zao zirekodiwe.

Hata hivyo, Gachagua ambaye alifika katika kituo cha Shule ya Msingi ya Sagana iliyopo eneo bunge la Mathira saa 7 asubuhi ili kupiga kura, alifurahishwa na mchakato wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka.

Mbunge huyo wa Mathira, aliongozana na mkewe Dorcas Rigathi na shangazi yake mzee ambaye alikuwa na matatizo ya kimwili ambaye alisaidiwa kupiga kura na wahudumu, huku Gachagua akiwataka Wakenya kujitokeza kwa wingi na kupiga kura.

Simba Day yampagawisha Cesar Manzoki
Willson Oruma: Zoran Maki ajirekebishe mapema