Watu thelathini wameripotiwa kupoteza maisha baada ya bomba la mafuta kulipuka Kusini-Mashariki mwa Nigeria.

Tukio hilo lilitokea mwishoni mwa wiki hii katika mji wa Aba, chanzo kikielezwa kuwa ni jaribio la wizi wa mafuta kupitia bomba hilo ambalo sehemu yake inamilikiwa na kampuni ya Serikali ya Pipeline & Marketing, kwa mujibu wa tamko la Serikali lililotolewa jana.

“Tukio hilo lilitokea majira ya saa saba na nusu usiku. Watu walioteketea kwa moto ni zaidi ya 30, na watu wengine wengi ambao idadi yao kamili haijajulikana wamejeruhiwa,” manusura wa tukio hilo, Mnamdi Tochukwu ameviambia vyombo vya habari, akiwa amelazwa hospitalini.

Msemaji wa Shirika la Nigerian National Petroleum, Ndu Ughamadu alisema kuwa waathirika ni watu ambao waliokuwa wanaiba mafuta kutoka kwenye bomba hilo.

“Siwezi kutoa idadi ya majeruhi kwa sasa, lakini mlipuko ulisababishwa na wezi wa mafuta waliokuwa wamedukua mkondo wa mafuta ya petrol,” Ughamadu ameiambia AFP.

Matukio ya mlipuko wa bomba la mafuta katika maeneo ambayo mafuta hupitia yamekuwa yakiripotiwa katika maeneo mbalimbali nchini Nigeria kwa miaka kadhaa.

Msako wa waliomteka Mo Dewji washika Bahari ya Hindi
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Oktoba 14, 2018