Ndege ya Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) iliyoondoka Dar es salaam saa 12:00 kuelekea Bukoba mkoani Kagera kupitia Mwanza, imekwama jijini Mwanza baada ya kupata hitilafu.

Kuharibika kwa ndege hiyo kumesababisha abiria waliokuwa wakielekea Bukoba kukwama hadi sasa bila kuelezwa hatima yao, hali iliyopelekea abiria hao kuujia juu uongozi wa shirika hilo jijini Mwanza.

Akizungumza kwa simu, mmoja wa abiria ambaye alikuwa anaelekea kwenye msiba wa shemeji yake kutokea Mwanza, Muhiddin Khalid alisema alitakiwa kuripoti saa 12:15 asubuhi na walipanda ndege saa 2:15 asubuhi walitakiwa kufika Bukoba saa 3:15.

“Baada ya kupanda tulikaa muda mrefu ndani bila ndege kuondoka, baadaye tumeambiwa tushuke ndege mbovu, hivyo mpaka sasa saa 6:05 tupo hapa hatujui kinachoendelea tumeambulia kikombe cha chai,” amesema Khalid.

Hata hivyo, Meneja wa ATCL Uwanja wa Ndege wa Mwanza, Theonestina Alchard amesema kuwa ni masuala ya kiufundi hivyo hawezi kuzungumzia zaidi kwa sababu yeye siyo msemaji wa kampuni.

Video: Wafuasi wa Jubilee waandamana Kenya
Zitto: Nimeumia sana nyumba yangu kuteketea kwa moto