Boomplay App inayoongoza barani Afrika kwa huduma ya kusikiliza na kupakua muziki imefanya kongamano lake la kwanza kwa ajili ya wasanii nchini Tanzania.

Katika kongamano hilo, Meneja wa Boomplay Tanzania, Natasha Stambuli amesema kuwa ni jambo la muhimu kuwawezesha wasanii na uzalishaji wa muziki (Production) na usambazaji wa muziki kidigitali (Digital Distribution).

“Boomplay tunatambua changamoto mbalimbali zinazowakabili wasanii, kama kupata muda wa studio, kurekodi video zenye ubora wa kimataifa na mengine mengi, Tumeingia mkataba na Wanene Entertainment ili kuwezesha wasanii kuondokana na matatizo hayo.”amesema Stambuli

Aidha, amesema kuwa Boomplay Barani Afrika ina ofisi katika nchi za Tanzania, Kenya, Nigeria na Ghana. hivyo amewataka wasanii kuchangamkia fursa ambayo itawapatia mtandao mkubwa wa kuwaunganisha na wasanii kutoka nchi mbalimbali.

Kongamano hilo lilijumuisha jopo la wataalamu mbalimbali katika tasnia ya muziki akiwemo, Martha Huro- Meneja wa Boomplay Kenya, Lupakisyo Mwambinga- Mkuu wa Idara Ya Sheria COSOTA, Nahreel kutoka Navy Kenzo, Moses Range- Muanzilishi DEMO Innovators, Japhet Kapinga- Meneja Maudhui Boomplay na kuratibiwa na msanii wa miondoko ya Hip Hop, Wakazi.

Boomplay ambayo awali ilikuwa ikifahamika kama Boomplayer, ni jukwaa linalotoa huduma ya kusikiliza na kupakua (download) muziki ambayo ipo chini ya umiliki wa kampuni ya Transsnet Music Limited.

Malengo ya App hiyo ni kutengeneza jukwaa kubwa na la kutegemewa na wasanii na wazalishaji wa muziki katika usambazaji wa kazi hizo za sanaa, ambapo watumiaji wake wanaweza kusikiliza na kuangalia video bure, kwa kujisajili.

 

Watumiaji dawa za kulevya wapungua Tanzania
Benki ya Wakulima TADB kukifufua kiwanda cha TANICA mkoani Kagera