Boti imeripotiwa kuzama ndani ya Ziwa Victoria, Jumamosi usiku pembeni kidogo mwa jiji la Kampala nchini Uganda ikiwa na abiria 90 waliokuwa wanakwenda kwenye hafla binafsi katika hoteli ya kifahari ya ufukweni.

Kwa mujibu wa BBC, miili 29 imepatikana hadi sasa ambapo Mamlaka imeeleza kuwa idadi ya waliopoteza maisha inaweza kuongezeka wakati uokoaji na utafutaji ukiendelea. Watu kadhaa wameendelea kuokolewa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Rais Yoweri Museveni, boti hiyo ilikuwa imejaza watu kupita kiasi, kwani uwezo wake ni kubeba watu 50. Hata hivyo, Rais Museveni amesema kuwa boti hiyo iliyokuwa inamilikiwa na Templa Bissase na mkewe haikuwa na leseni ya kufanya shughuli ya usafirishaji.

Aidha, ripoti ya awali ya Mamlaka husika zilizochapishwa kwenye gazeti la The Monitor la nchini humo, zimeeleza kuwa meli hiyo iliyokuwa imewabeba watu wanaokwenda kwenye starehe, ilikuwa na muziki wenye sauti kubwa kupita kiasi, abiria wengi walikuwa wamelewa na hawakuvaa jaketi maalum za kuwasaidia kuelea (life jackets).

Imeelezwa kuwa kutokana na sauti ya muziki mkubwa iliyokuwa inasikika, abiria hawakusikia tangazo la tahadhari lililotolewa na nahodha wa boti hiyo.

Kati ya waliookolewa ni pamoja na mwanamuziki Iryn Namubiru pamoja na Prince Daudi Kintu Wassajja ambaye ni ndugu wa Mfalme wa Buganda.

Rais wa Zimbabwe azungumzia afya ya Mugabe, ‘hatembei’
Urusi yateka meli za Ukraine, yaziba njia ya bahari