Mlinzi wa kulia wa timu ya taifa ya Brazil, Danilo Luis Da Silva ataukosa mchezo wa robo fainali hii leo dhidi ya Ubelgiji baada ya kuumia kifundo cha mguu wa kulia wakati akifanya mazoezi kujianda na mchezo huo.

Chama cha soka nchini Brazil kimedhibitisha taarifa hizo na kueleza kuwa Danilo hatoweza kupona na kucheza mchezo wowote kwenye michuano ya kombe la dunia msimu huu nchini Russia.

Aidha, Imeelezwa kuwa mchezaji huyo wa klabu ya Manchester City atabaki kikosini wakati akiendelea kupatiwa matibabu.

Danilo ambaye alikuwemo kwenye kikosi cha Brazil kilichocheza mchezo wa kwanza dhidi ya Switzerland, na baadae alikosa michezo miwili iliyofatia dhidi ya Costa Rica na Serbia kutokana na kusumbuliwa na majeraha.

Hata hivyo, baada ya kupona alijumuishwa kwenye kikosi cha Brazil kilichoshinda 2-0 dhidi ya Mexico kwenye mchezo wa hatua ya 16 bora.

Brazil itashuka uwanjani leo Ijumaa kucheza mchezo wa robo fainali dhidi ya ubeligiji huku mchezo mwengine ukiwakutanisha Ufaransa dhidi Uruguay kwenye uwanja wa Nizhny Nogorod nchini Russia.

 

Moto wa Lugola wamchoma Kamishna Magereza, amtimua
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Julai 6, 2018