Spika wa bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania Job Ndugai amesema Bunge litashirikiana na Tume ya haki za binadamu na utawala bora (THBUB), katika mambo mbalimbali ili kusimamia na kuhamasisha masuala ya haki za binadamu nchini.

Ndugai ameyasema hayo Wilayani Kongwa Mkoani Dodoma alipokutana na Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu aliyemtembelea katika ofisi yake ya jimbo iliyopo Wilayani humo.

Akiongea katika kikao hicho Ndugai alimueleza Mwenyekiti kuwa THBUB ni taasisi muhimu ambayo imepewa dhamana ya kusimamia haki za binadamu nchini na kwamba imekuwa ikifanya kazi nzuri licha ya uwepo wa changamoto katika kutekeleza majukumu yao.

“Natambua eneo ambalo tume inalifanyia kazi ni gumu maana linahusiana na masuala ya usimamizi wa haki za watu lakini changamoto hizo zisiwakatishe tamaa pale mtakapokuwa na jambo lolote msisite kuwasiliana na ofisi ya Bunge ili kushirikiana kuzitatua,” amefafanua Ndugai.

Ndugai ameongeza kuwa THBUB imekuwa ikikutana na changamoto mbalimbali ikiwemo migogoro ya ardhi, migogoro ya wakulima na wafugaji lakini anaamini itaisaidia serikali katika kuipunguza kama sio kuimaliza matatizo yaliyopo nchini.

Kuhusu mapungufu mbalimbali ya sheria Spika Ndugai amemueleza Mwenyekiti wa tume hiyo kuwa wasisite kuwasilisha kwa ofisi ya Bunge mapendekezo yoyote endapo wataona kuna sheria kandamizi ili ziweze kuwasilishwa katika vikao na kufanyiwa marekebisho.

“Naamini wakati wa kushughulikia migogoro huwa mnakutana na changamoto za vipengele vya sheria nadhani hii siyo sawa wala sio haki sasa mkiona zipo sheria kandamizi msisite kuwasilisha Bungeni ili katika vikao vyetu tuzijadili na kuzifanyia marekebisho hili tutalizingatia,” amesisitiza Spika Ndugai.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa tume ya haki za binadamu na utawala bora Jaji Mathew Mwaimu amemueleza Spika Ndugai kuwa dhamana waliyopewa na Rais John Magufuli ni kubwa na hivyo wanaahidi kuitendea haki kwa kufanya kazi kwa bidii.

Mwenyekiti huyo wa Tume alifika kumtembelea na kujitambulisha kwa Spika wa Bunge Job Ndugai tangu kuapishwa kwake Novemba 4, 2019 akiongozana na Makamu wake Mohamed Khamis Hamad na Makamishna Dkt. Fatma Rashid Khalfan, Thomas Masanja, Amina Talib Ali na Nyanda Josiah Shuli.

Video: Muhimbili kuanza kupandikiza mimba, Watu 11 nyuma ya uraisi wa Mkapa
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Novemba 20, 2019