Burundi imeonesha kukasirishwa na kitendo cha Serikali ya Ufaransa kupitia taasisi yake kutoa punda kama zawadi yake kwa wanakijiji wa Gitega nchini humo.

Punda hao walionunuliwa nchini Tanzania waliwasilishwa kwa wanakijiji hao kama sehemu ya mradi wa kuwasaidia wanawake na watoto kusafirisha mazao ya kilimo, maji pamoja na kuni.

Hata hivyo, mshauri wa Rais ameitaja zawadi hiyo kama matusi kwa taifa hilo la Afrika Mashariki, akisema kuwa imebeba ujumbe mbaya kutoka Ufaransa.

Gabby Bugaga, msemaji wa seneti ya Rais pia aliandika ujumbe kwenye Twitter akieleza kuwa, “Ufaransa wanatuchukua kwa punda”.

“Kuweni wakweli, punda ni ishara ya ubora au ubovu,” aliongeza kwenye tweet yake.

Jumapili iliyopita, Waziri wa kilimo wa Burundi, Deo Guide Rurema aliwataka watendaji kuhakikisha wanarudisha haraka punda wote waliowasilishwa kama zawadi kwa wanakijiji, akiongeza kuwa usambazaji wake haukufuata taratibu.

Alhamisi iliyopita, mradi huo ulizinduliwa na Balozi wa Ufaransa nchini Burundi, Laurent Delahousse ambaye aliusifia.

Mwanadiplomasia wa Ulaya ambaye alizungumza na shirika la habari la AFP kwa masharti ya kutotajwa jina alisema kuwa uamuzi huo wa Burundi ni kulipiza kisasi kutokana na kauli ya Ufaransa ya hivi karibuni ya kukosoa uendeshwa na matokeo ya kura za maoni ambayo yanampa nafasi Rais Pierre Nkurunziza kuongeza mihula miwili itakayokamilika mwaka 2034.

Ajali ya pikipiki yaua baba mama na mtoto Rukwa
Lukuvi afikisha ujumbe mzito kwa wamiliki wa ardhi