Bwawa ambalo ukuta wake ulibomoka Jumatano hii nchini Kenya na kuua zaidi ya watu 40 lilijengwa kinyume cha sheria na taratibu, kwa mujibu wa Mamlaka ya Vyanzo vya Maji nchini humo.

Uongozi wa Mamlaka ya Vyanzo vya Maji imeeleza kuwa ujenzi wa bwawa hilo la Solai lililoko umbali wa kilometa 190 kutoka jiji la Nairobi haukufuata sheria na kwamba waliohusika watachukuliwa hatua kali.

“Mabwawa haya yote, hakuna hata moja lililokuwa na kibali, yote yamejengwa kinyume cha sheria,” alisema Elizabeth Luvonga, msemaji wa Mamlaka hiyo.

Kufuatia kubomoka kwa ukuta wa bwawa hilo, maji yalivamia makazi ya watu na kubomoa zaidi ya nyumba za familia 145, kuua watu, mifugo na kusababisha uharibifu mkubwa wa vitu na miundombinu.

Zaidi ya miili 32 ilipatikana siku iliyofuata, huku kati ya hiyo miili 11 ilitajwa kuwa ya watoto na wanawake. Waokoaji wameendelea kupata miili zaidi kwenye tope na inahofiwa kuwa huenda idadi ya waliokufa ikaongozeka.

Hata hivyo, meneja wa bwawa hilo , Vinoj Kumar alikanusha taarifa hizo za kutokuwa na kibali, alipofanya mahojiano na Reuters.

“Mabwawa haya yote yalijengwa miaka 15 hadi 20 iliyopita. Hakuna hata moja ambalo haliko kisheria,” alisema Kumar.

Mwendesha Mashtaka wa Serikali ametangaza kuanza uchunguzi kuhusu tukio hilo kwa lengo la kuwachukulia hatua watakaobainika kukiuka sheria.

 

Neymar: Ninahitaji sana kuichezea timu yangu
Dani Alves kuzikosa fainali za kombe la dunia