Shirikisho la soka barani Afrika CAF limemsafishwa mwamuzi kutoka nchini Liberia Jerry Yekeh, baada ya kutuhumiwa kuhusika na masuala ya kupokea rushwa akiwa katika majukumu ya kusimamia sheria 17 za mchezo wa soka.

Yekeh alikua miongoni mwa waamuzi waliotajwa kwenye uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari za uchunguzi kutoka nchini Ghana Anas Aremeyaw Anas.

Mwamuzi huyo alituhumiwa kuhusika kuchukua rushwa wakati wa fainali za mataifa ya Afrika ya magharibi zilizochezwa mwaka 2017, lakini CAF wamefuatilia kadhia hiyo na kubaini uchunguzi uliofanywa na mwandishi Anas, ulikua haujakidhi vigezo vya kumtia hatiani Yekeh.

Mwamuzi huyo mwenye beji ya FIFA alikua ameshahukumiwa na kamati ya nidhamu ya shirikisho la soka barani Afrika CAF mwezi Julai mwaka huu, lakini hatua ya kukata rufaa imemsaidia na kuthibitika hakua na kesi ya kujibu.

Ushahidi wa video iliyopigwa ambayo ilitumika kumfungia mwamuzi huyo, umeshindwa kuweka wazi ukweli wa Yekeh kuhusiska katika sakata hilo, kutokana na anaedaiwa kuwa yeye, kutoonekana vyema kupitia video iliyopigwa na mwandishi Anas.

Kufuatia maamuzi hayo, chama cha soka nchini Liberia kimeupongeza uamuzi wa CAF uliochukuliwa dhidi ya mwamuzi ambaye ni raia wa taifa hilo, na sasa anarejea katika majukumu yake ya usimamizi wa sheria 17 za mchezo wa soka.

Mwamuzi kutoka Kenya Aden Marwa tayari ameshafungiwa na CAF kwa kutumia uthibitisho wa picha za televisheni zilizopigwa na mwandishi Anas, huku wengine kumi kutoka Ghana wakikutana na rungu hilo.

Kisa cha wazazi wa mwanafunzi darasa la tatu kutiwa mbaroni
Video: 'Producer' wa Tanzania ashushiwa kichapo Kenya