Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad amezungumzia uamuzi wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa kutofanya naye kazi.

Amesema kuwa Bunge linapaswa kuangalia athari ya uamuzi wake kwani anaamini inaweza kuwa chanzo cha tatizo lingine kubwa zaidi katika siku za usoni.

“Tukifanya uamuzi ambao hatujatazama athari zake, linaweza kuwa tatizo kubwa zaidi badala ya kupata solution (utatuzi),” CAG aliiambia TBC kwa njia ya simu.

“Mimi nafikiri tukae chini tutazame, halafu tuone athari ni zipi ili kuepuka matatizo ambayo tunaweza kuyasababisha… wasiwasi wangu ni kwamba huenda linaweza likaja kuwa tatizo kubwa zaidi kuliko linavyoonekana sasa,” aliongeza.

Aidha, Profesa Assad ambaye yuko nje ya nchi, ametoa rai kuwa hansadi za mahojiano kati yake na Kamati ya Bunge ziwekwe wazi ili kila Mtanzania aone jinsi ambavyo alijibu maswali husika.

Jana, Bunge la Jamhuri ya Muungano lilipitisha uamuzi wa kutofanya kazi na CAG, baada ya kujiridhisha kuwa kauli yake kuhusu ‘udhaifu wa bunge’ aliyoitoa alipofanya mahojiano na kituo cha radio cha kimataifa akiwa nchini Marekani ililenga kulidhalilisha Bunge.

Kamati ya Bunge ilieleza kuwa katika mahojiano, CAG aliweka msimamo kuwa kauli yake ilikuwa sahihi na kwamba ataendelea kulitumia neno ‘udhaifu’ kwani anaamini halina makosa.

JPM awaweka kikaangoni wakurugenzi, 'Ole wake aniombe hela'
LIVE: Rais Magufuli akiendelea na ziara ya kikazi mkoani Mtwara