Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole amesema kuwa njia pekee ya CCM kulipa wema kwa wananchi ni viongozi wake kufanya kazi kwa bidii na ubunifu ili kuleta maendeleo nchini.

Amesema kuwa wananchi wamekiamini Chama na kukipa ridhaa ya kuongoza Serikali zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutokana na usimamizi na utekelezaji mzuri wa Sera zake kwa jamii.

Ameyasema hayo katika hafla ya kukabidhi mipira ya kusambazia maji safi na salama kwa wananchi wa Jimbo la Tunguu Wilaya ya Kati Unguja.

Polepole amewasifu viongozi hao wa chama hicho kwa juhudi za kuwatumikia wananchi, ambao ni Mbunge wa Jimbo hilo, Khalifa Salum Said na Mwakilishi wa Jimbo hilo Simai Mohamed Said kuwa wametoa mipira hiyo kwa lengo la kumaliza changamoto ya ukosefu wa huduma za maji.

Aidha, amesema kuwa viongozi wa Chama na Serikali hasa Wabunge, Wawakilishi na Madiwani nchini wanatakiwa kuendeleza utamaduni wa kufanya kazi na kuwapelekea wananchi maendeleo na sio ahadi za uongo.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Jimbo la Tunguu, Simai Mohamed Said,amesema kuwa ataendelea kuimarisha huduma mbalimbali za kijamii na kiuchumi ndani na maeneo jirani ya Jimbo hilo.

Naye Mbunge wa Jimbo hilo, Khalifa Salum Said, amesema kuwa viongozi hao wamejipanga kumaliza kero ya upungufu wa maji safi na salama katika Vijiji mbalimbali vilivyomo katika Jimbo la Tunguu.

 

Arsene Wenger aikana AC Milan
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Novemba 7, 2018