Uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Njombe umempongeza mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Iringa, Abel Nyamahanga kwa kuchaguliwa na wanachama kuwa mwenyekiti wa CCM mkoa wa Iringa.

Pongezi hizo zimetolewa na katibu wa siasa na uenezi wa chama cha mapinduzi CCM mkoa wa Njombe, Erasto Ngole alipomtembelea mwenyekiti huyo Ofisini kwake mara baada ya kuchaguliwa na wanachama mkoani Iringa siku chache zilizopita.

Akizungumza na mwenyekiti huyo wa CCM mkoa wa Iringa, Erasto Ngole amemueleza kuwa historia ya mkoa wa Njombe imetokana na mkoa wa Iringa hivyo ushirikiano uliopo kati ya mikoa hiyo miwili umeendelea kudumishwa na wananchi wake ambao wanatambua historia hiyo hasa katika kusaidiana kuujenga mkoa wa Iringa.

“Mwenyekiti nikupongeze sana kwa kuchaguliwa tena ukiwa bado kijana kabisa naamini tutaendelea kushirikiana katika masuala mbalimbali ya kulijenga taifa letu, natambua thamani ya mkoa wa Iringa iliyopo katika mkoa wetu wa Njombe hasa historia yetu tulikotoka ndio maana leo nimefika hapa,”amesema Ngole

Aidha, kwa upande wake mwenyekiti wa chama cha mapinduzi CCM mkoa wa Iringa, Abel Nyamahanga amemshukuru katibu wa siasa na uenezi mkoa wa Njombe kwa kusafiri hadi Iringa kwaajili ya kumpongeza na kusema kuwa jambo hilo limemfurahisha na kumtia moyo wa ukakamavu katika kutekeleza majukumu yake ya kusimamia serikali katika kutekeleza ilani ya CCM katika mkoa wa Iringa.

Hata hivyo, kikao hicho kifupi cha mazungumzo kilihudhuriwa na katibu wa CCM mkoa wa Iringa, Brow Mwangomale pamoja na katibu wa siasa na uenezi wa mkoa huo, Mwinyikheri Baraza ambao kwa pamoja wamesema kuwa wanatambua mchango wa katibu wa siasa na uenezi CCM mkoa wa Njombe, Erasto Ngole katika jamii.

 

Watu 5 wafariki dunia shambulio la hoteli Nairobi
Al-shabab wakiri kuhusika shambulio Nairobi