Teknolojia mpya ya habari na mawasiliano inamchango mkubwa sana kwenye uchaguzi wa mwaka huu, bila shaka imeongeza chachu ya ushindani kutokana jinsi ambavyo habari zinasambaa kwa muda mfupi ukilinganisha na chaguzi zilizopita.

Hata hivyo, teknolojia hii imeibua wasiwasi mwingine kuwa huenda ikawa inatumika katika kufanya udanganyifu kwa kuchezea (manipulate) picha zinazoonekana kuwa za mikutano ya baadhi ya wagombea.

Dr. Emmanuel Nchimbi, mjumbe wa kamati ya kampeni ya CCM ameeleza kwa nyakati tofauti kuwa picha zinazoonekana za mikutano ya mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa hazina uhalisia bali zimehaririwa ili kuonekana kuwa alikuwa na watu wengi kwenye mikutano yake.

Baadhi ya makada wa CCM kupitia mitandao ya kijamii wamekuwa wakieleza kuwa picha inayosambaa ikionesha mafuriko ya Lowassa hivi karibuni jijini Arusha sio ya kweli bali ni umati wa watu katika nchi moja ya Afrika Magharibi.

Huu ni muendelezo wa tuhuma za CCM dhidi ya Chadema kuhusu picha hizo kwani Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Jakaya Kikwete aliwaeleza wananchi waliohudhuria katika uzinduzi wa kampeni zake katika uwanja wa Jangwani, Dar es Salaam, kuwa wasitishwa na picha za Chadema kwa kuwa zimehaririwa na sio kweli.

“Wamechukua picha nyingine za mikutano ya Dk. Slaa, wanaunganisha, waambieni waje waone picha halisi,” alisema.

Hata hivyo, Chadema na Ukawa kwa ujumla walimjibu mwenyekiti huyo wa CCM katika siku ya uzinduzi wa kampeni zao uliohudhuriwa na maelfu ya watu kwa kumtaka aione picha halisi ili aamini kuwa hakuna uhariri katika picha anazoziona.

Je, ni kweli picha za Chadema zinahaririwa? Bado Dar24 haina jibu la moja kwa moja. Swali hilo tunawaachia watazamani wa mikutano hiyo hasa waliohudhuria.

Mbowe Amfungulia Mlango Dk. Slaa, Atoa Siri Ambayo Hakumwambia Lowassa
Diamond, Vanessa Mdee Wang’ara Marekani Tuzo Za AFRIMA 2015